24.8 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

‘Chagueni viongozi watakaotuvusha 2024/25’

Na Mwandishi Wetu, Mtanzania Digital

Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Ilala kimewataka wanachama kuchagua viongozi wenye dhamira ya kukitumikia na kuepuka wale wanaotaka uongozi kwa manufaa yao binafsi.

Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Ilala, Ubaya Chuma, akikata keki wakati wa maadhimisho ya miaka 45 ya kuzaliwa kwa chama hicho yaliyofanyika katika Kata ya Mnyamani.

Akizungumza wakati wa sherehe za maadhimisho ya miaka 45 ya chama hicho ambazo kiwilaya zilifanyika katika Kata ya Mnyamani, Katibu wa CCM Wilaya ya Ilala, Idd Mkowa, wanahitaji viongozi ambao muda wote watakuwa wanaumia kama chama hakiendi vizuri.

Aidha amewataka makatibu wa matawi, kata, kamati za siasa ambako watachuja wagombea kuzingatia kaulimbiu inayohimiza uadilifu ili kupata viongozi bora.

“Tunahitaji tupate viongozi ambao hawatokani na figisu ndiyo maana ya uadilifu, tukikosea kuweka viongozi wazuri tambueni kwamba 2024/2025 kazi tutakuwa nayo, kwa sababu wako wanaoomba uongozi kwa manufaa yao binafsi lakini kiongozi ambaye anakuja kwa dhamira ya kukitumikia chama matunda yake tutayaona 2024/2025.

“Wanachama mnawafahamu, viongozi mnawafahamu hivyo niwaombe sana tuwape nafasi wale ambao hawana uroho wa madaraka, hawana tamaa hawaingii kuomba uongozi kwa ajili ya kwenda kupiga kura za maoni,” amesema Mkowa.

Naye Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Ilala, Ubaya Chuma, amewataka wanachama kujitokeza kwa wingi kugombea nafasi mbalimbali kwani hakuna mwenye nafasi na kwamba kila mwanachama ana haki ya kugombea.

“Niwaombe sana hiki ndio kipindi cha nongwa cha kusemana vibaya, acheni kila mmoja kwa nafasi aliyokuwa nayo ataona namna gani anawiwa kugombea, tusiwabeze wenzetu tuwaache wakagombee vikao na mikutano mikuu vitaamua.

“Watu mmeanza kampeni na wengine mmeanza kukamuliana ndimu, tuyaache mambo hayo uongozi unatoka kwa Mungu, kila mwenye nia ya kugombea akagombee,” amesema Chuma.

Aidha amesisitiza kwa wanachama na viongozi kuwa waadilifu ili kuweza kupata viongozi bora sambamba na kumuunga mkono Rais Samia Suluhu Hassan kutokana na kazi kubwa anazozifanya.

Maadhimisho hayo yalienda sambamba na uzinduzi wa ujenzi wa ofisi za CCM Kata ya Mnyamani na tawi la Mji mpya inayojengwa kwa ufadhili wa Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Mji mpya.

Mwenyekiti wa CCM Kata ya Mnyamani, Mbaraka Mwinyimvua, amesema ujenzi wa ofisi hizo unalenga kusaidia jitihada za Mwenyekiti wa Taifa wa chama hicho, Rais Samia ambaye anaendelea kukijenga chama kizidi kuwa imara.

Aidha katika sherehe hizo chama hicho kiliwapokea wanachama wapya kutoka CUF na vyama vingine akiwemo aliyewahi kuwa Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Mnyamani, Jabir Sanze.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles