MKUU wa Kituo cha Polisi cha Ngarenairobi wilayani Siha mkoani Kilimanjaro, Mkaguzi Msadizi wa Polisi , Morisi Sungu amefariki dunia kwa ajali ya pikipiki, baada ya kugongana na gari la abiria katika barabara ya Bomang’ombe Sanya Juu.
Ajali hiyo, iliyohusisha pikipiki yenye namba za usajili T389 DRW ambayo ilikuwa ikiendeshwa na marehemu Sungu na gari la abiria lenye namba za usajili T 149 DEY aina ya Toyota Hiace iliyokuwa inaendeshwa na Peter Ulomi (30) mkazi wa Bomang’ombe.
Akizungumza eneo la tukio jana, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro,Wilbroad Mtafungwa alisema ajali hiyo ilitokea eneo la Kwa Mama Sawa saa 12:15 asubuhi wakati marehemu akielekea kazini kwake Ngarenairobi.
Alisema ajali hiyo ilichangiwa na mwendo kasi wa dereva wa gari la abiria ambalo lilitaka kupita gari jingine bila kuchukua hadhari .
“Tunafanya uchunguzi wa ajali hii, mashuhuda wametwambia mwendo kasi umechangia kifo cha askari mwenzetu,”alisema Kamanda Mtafungwa.
Alisema dereva wa gari hilo, anashikiliwa na polisi kwa uchunguzi zaidi na atafikishwa kwenye vyombo vya sheria kwa hatua zaidi. Mmwili wa marehemu umehifadhiwa Hospitali ya Wilaya ya Hai.