24.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Balozi Haule: Agizo la Rais linatekelezeka

unnamed (14)Na Hamisa Maganga, Nairobi

BALOZI wa Tanzania nchini Kenya, John Haule, amesema agizo la Rais Dk. John Magufuli la kuwataka mabalozi kuwawakilisha viongozi wanaotakiwa kwenda nje ya nchi kikazi linatekelezeka, japo wanakutana na changamoto kadhaa.

Akizungumza na waandishi wa habari wa Tanzania walioko nchini hapa juzi,Balozi Haule alisema  yeye na mabalozi wengine wanaunga mkono agizo hilo, lakini kuna changamoto ambazo balozi zinakabiliana zinahitaji ufumbuzi ili kufikia malengo.

Alisema moja ya changamoto kubwa ni  balozi nyingi kukabiliwa na upungufu wa watumishi, jambo ambalo linawarudisha nyuma.

Alisema  katika balozi za Tanzania zilizopo nchi mbalimbali duniani, kuna maofisa wamesomea masuala ya kidiplomasia, lakini hawatoshi kwa kuwa idadi yao ni ndogo.

Alisema maofisa hao, wanapaswa kuungwa mkono na kada zingine kama wachumi na watu wenye utaalamu wa biashara.

“Tunajivunia ushirikiano wetu wa kibiashara kati ya Kenya na Tanzania, hatuna ofisa biashara angetusaidia kuratibu vizuri masuala mbalimbali ya kibiashara na taasisi zilizopo.

“Tunaweza kupokea maelekezo kutoka nyumbani yanayohusu masuala ya kibiashara, wakati mwingine tunakwama namna ya kufikisha ujumbe kwa wahusika wenzetu,”alisema Balozi Haule.

Alisema mikutano mingi inafanyika Nairobi na katika miji kama Naivasha na Mombasa ambako ni mbali na uwezo wa kufika balozi ni mdogo.

Alisema ili kutekeleza utaratibu huo,wanahitaji fedha na magari ya uhakika.

“Changamoto hizi tumezifikisha wizarani, nina imani muda si mrefu zitafanyiwa kazi ili kutekeleza maagizo tunayopewa kwa urahisi zaidi,”alisema.

Kuhusu uongozi wa Rais Dk. Magufuli, Balozi Haule alisema Tanzania ilichelewa kumpata kiongozi kama huyo kutokana na kujali maslahi ya nchi yake.

Alisema kabla ya kuingia madarakani kwa Rais Magufuli, nchi ilikuwa inakwenda bila uhakika wa safari.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles