SERIKALI imeagiza mifugo yote ambayo ni ya raia wa kigeni kutoka nchi jirani na ile ya wazawa kutolewa haraka katika mapori ya akiba na hifadhi za misitu.
Kauli hiyo, imetolewa jana na Waziri wa Maliasili na Utalii, Profesa Jumanne Maghembe wakati wa ziara ya kikazi wilayani Bukombe mkoani Geita.
Alisema mifugo yote ya wazawa, inatakiwa pia kutolewa katika mapori ya akiba na hifadhi za misitu kwa hiari na ifikapo Juni 15, mwaka huu kusiwepo na mifugo ndani ya hifadhi.
Alisema mifugo itakayobaki katika hifadhi hizo, itakuwa imevunja sheria na wahusika watashtakiwa na mali zao zote zitaifishwa. “Doria ziendelee ili kuhakikisha maelekezo haya yanatekelezwa ipasavyo,” alisema.
Kuhusu ng’ombe 454 waliokamatwa na kuzuiliwa hifadhini, Waziri Maghembe alisema kesi yake inaendelea na kuwa suala hilo litasimamiwa na Mkuu wa Mkoa wa Geita, Meja Jenerali mstaafu, Ezekiel Kyunga.
Alisema operesheni za kuondoa mifugo na makazi ndani ya mapori ya akiba na hifadhi za misitu, zifanyike kwa kushirikisha kamati za ulinzi na usalama za mikoa na wilaya husika ili kuondoa malalamiko ya viongozi kula rushwa na kunyanyasa wananchi.
Alisema kuna changamoto kubwa zinazoathiri ustawi wa maliasili katika maeneo yaliyohifadhiwa, kuwa ni ujangili na ulishaji wa mifugo.
Akitoa mfano, alisema katika pori la akiba la Moyowosi/Kigosi peke yake, kuna zaidi ya ng’ombe milioni mbili ambao wamesababisha uharibifu mkubwa unaofikia asilimia 30 ya vyanzo vya Mto Malagarasi, ambacho ndiyo chanzo kikubwa cha maji cha Ziwa Tanganyika.