24.5 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

ATHARI ZA KUSUKA, KUWEKA DAWA KWA KINA DADA

Na MWANDISHI WETU

NI dhahiri kwamba kati ya wanawake kumi, mmoja tu ndiye unayeweza kumkuta akiwa na nywele zake za asili, waliosalia  utawakuta aidha wamesuka, wameshonea nywele za bandia (weaving) au wameweka dawa.

Wengi hufanya hivyo kwa sababu ya kusaka urembo na kupendezesha muonekano wao.

Utafiti uliofanywa na wataalamu wa kliniki ya Cleveland iliyoko nchini Marekani, umebaini kuwa wanawake wanaobadili nywele zao wako katika hatari ya kupoteza nywele zao za asili.

Watafiti hao wanaeleza katika matokeo ya utafiti wao uliowahusisha wanawake 326 wenye asili ya Kiafrika (African-American) ambao baadae ulichapishwa katika jarida la ‘Archives of Dermatology’.

Wanaeleza kwamba mwanamke anayesuka mara kwa mara hujiweka kwenye hatari zaidi ya kunyonyoka nywele zake za asili ikilinganishwa na yule anayesuka mara chache.

Kwamba, urembo huo uchangia kwa kiasi kikubwa kuongeza kiwango cha maambukizi kwa kuzaliwa bakteria ambao uharibu mfumo mzima wa ukuaji wa nywele na kuharibu ute ute muhimu unaozuia mba.

Kati ya wanawake 326 waliohusishwa katika utafiti huo, asilimia 59 waligundulika kuwa tayari wameathiriwa na tatizo hilo kwa kiasi fulani na wengine wakiwa wameathiriwa kwa kiasi kikubwa zaidi.

Matokeo hayo yanaeleza kwamba wanawake waliopoteza nywele zao za asili walikuwa wengi zaidi na wale waliopatwa na maambukizi ya bakteria.

“Karibu asilimia 20 ya wanawake walikutwa wamepoteza nywele na wana maambukizi ya bakteria walioshambulia ngozi zao za kichwa, ikilinganishwa na asilimia 11.4 ya wanawake wote katika utafiti ambao walipoteza nywele pekee.

Kwa mujibu wa utafiti huo, asilimia 96 ya wanawake wanaonyonyoka nywele ni wale waliotumia dawa za kulainisha nywele zao.

Wakati huo huo, asilimia 57 ya wanawake wanaonyoyoka nywele husababishwa na kusukia nywele bandia (rasta), ama kushonea nywele bandia.

Kwa upande wa ugonjwa wa kisukari, haukuonekana kuwapo kwa kiasi kikubwa miongoni mwa wanawake waliofanyiwa utafiti, lakini wengi walionyonyoka nywele ndiyo waliokutwa na ugonjwa huo kuliko wale ambao hawakunyonyoka nywele.

Mfano; ni asilimia 17.6 ya wanawake walionyonyoka nywele kwa kiasi kikubwa wamekutwa na ugonjwa wa kisukari aina ya pili (Type 2).

Tafiti zilizopita zinashauri kuwa tatizo hili (cicatricial alopecia) ni moja ya kichocheo cha mfumo wa chakula ambao unatakiwa kufafanua zaidi ni kwanini wanawake wote walionyonyoka nywele waliofanyiwa utafiti wamekutwa na ugonjwa huo wa kisukari aina ya pili (Type 2) kuliko wale wasionyonyoka nywele.

Utafiti huo unataja aina ya unyonyokaji ambapo nywele huanza kunyonyoka kuanzia kwenye ngozi kuzunguka kichwa. “Inaonyesha kuwa kunyonyoka nywele kumetokea zaidi kwa wanawake wa Kimarekani wenye asili ya Kiafrika,” umeongeza tafiti.

Kusukia nywele bandia (rasta) na kushonea nywele bandia pia ni mojawapo ya mitindo inayotumika zaidi miongoni mwa jamii ya wanawake wa Kimarekani wenye asili ya Kiafrika.

Utafiti huo umeongeza kuwa wengi wao wanaosuka nywele bandia hukaa nazo muda mrefu kati ya wiki mbili au hata mwezi kama sehemu ya kufidia gharama za ususi zilizizotumika.

Usukaji wa nywele hizo pia huwasababishia kuvutwa ambako kunachangia kwa kiasi kikubwa kuvurugwa kwa mfumo wa ukuaji nywele kwenye mizizi yake na hivyo kusababisha vidonda na hata makovu kwenye ngozi ya kichwa.

Watafiti hao wanafanya jitihada zaidi ili kufanya tafiti nyingine kwa lengo la kubaini iwapo matumizi ya dawa za kunyoosha nywele (relaxer) unaweza kuchangia upotevu wa nywele.

 

Daktari

Dk. Fredrick Mashili, Mtaalamu wa Fisiolojia ya Mazoezi na Homoni, ambaye pia ni Mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Sayansi na Tiba Muhimbili (MUHAS) anasema suala hilo lina ukweli.

“Muhas hatujafanya utafiti wa aina hii lakini tunajua kuwa zipo tafiti chache ambazo zimefanyika na tunazifuatilia kwa karibu.

“Lakini hadi nywele zinanyonyoka hutegemea na staili (mtindo) wa usukaji au dawa zinazotumika kupakwa kwenye nywele husika,” anasema.

Anasema kuwa namna nywele zilivyoumbwa na Mwenyezi Mungu, zinapaswa kuachwa wazi ili zipate hewa na mwanga wa kutosha.

“Kwa mfano; iwapo utayachukua majani na kuyafungia ndani ni lazima yatanyauka tofauti na yale yaliyoko nje, hivyo nywele asilia (natural) haziathiriki kama zile zinazotiwa dawa na au kusukwa.

“Kuvutwa kwa nywele husababisha wakati mwingine kichwa kuuma. Lakini athari zaidi huwapata wale wanaotumia dawa kwani baadhi ya kemikali zilizotumika kutengeneza dawa hizo hubakia na kunyonywa mwilini.

“Kwa mfano; kemikali ya steroid ambayo mara nyingi huwekwa kwenye vipodozi vya kujichubua na kemikali nyingine husababisha kunyonyoka nywele, na magonjwa mengine ya ngozi. Pia huleta dalili za ugonjwa wa kisukari,” anasema.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles