Rais Nieto aliliambia taifa katika hotuba yake kupitia runinga kwamba, “Nimesema tena na tena kwamba Mexico haitalipia ukuta huo.”
Aliongeza kuwa, ”Ninajuta na kushutumu uamuzi huo wa marekani wa kutaka kuendelea kujenga ukuta ambao umetugawanya kwa miaka badala ya kutuunganisha”.
Lakini pia Nieto amesema urafiki kati ya Mexico na raia wa Marekani utadumu mbali na kutafuta suluhu kuhusu tatizo la wahamiaji.
Hata hivyo, Rais Nieto kwa upande mwingine, anashinikizwa kufuta mkutano wake na Rais Trump unaotarajiwa kufanyika wiki ijayo mjini Washngton.
Kabla ya hapo, Trump tayari amesaini agizo la urais la kujenga ukuta kati ya Marekani na Mexico na amesisitiza kuwa Mexico itailipa Marekani kwa ukuta huo.
Hatua hiyo ni utekelezaji wa ahadi yake kubwa aliyoiweka wakati wa kampeni za uchaguzi yakuzuia wahamiaji haramu na wafanyabiashara wa dawa za kulevya, kwa kuongeza kuwa siku zao zimekwisha wao kuishi na kufanya uharibifu.
Amesisitiza kauli yake ya kutaka Mexico kulipia ukuta huo, licha ya Mexico kukataa kufanya hivyo.
Meya wa mji wa Mexico City Miguel Espinosa amesema kujengwa kwa ukuta huo, Marekani itajitenga yenyewe sio tu na Mexico bali na Amerika ya kusini yote.