25.2 C
Dar es Salaam
Friday, October 18, 2024

Contact us: [email protected]

Kama kadi ya Mkude batili, basi Yanga walibebwa

img_2619

Na ZAINAB IDDY,

KABLA ya kuchezwa kwa pambano la watani wa jadi, Simba na Yanga, habari kubwa ilikuwa ni timu ya soka ya taifa ya vijana chini ya miaka 17 ‘Serengeti Boys’, juu ya mechi ya mwisho ya kuwania kufuzu kwa Fainali za Mataifa ya Afrika kwa vijana, lakini ghafla upepo ukabadilika na kuwa Martin Saanya.

Serengeti Boys ilicheza Jumapili iliyopita dhidi ya Congo Brazzaville ugenini na kufungwa bao 1-0, matokeo yaliyoinyima nafasi ya kufuzu kwa fainali zitakazochezwa mwakani nchini Madagascar, ambapo wapinzani wao walifuzu kwa faida ya mabao mawili waliyofunga katika mchezo wa awali ugenini.

Upepo wa kuijadili Serengeti Boys ulianza kubadilika baada ya mwamuzi huyo kutoa uamuzi wa kutatanisha katika mchezo wa watani wa jadi katika soka nchini Simba na Yanga, ambapo kwa sasa yeye ndiye anazungumziwa zaidi kuliko jambo lolote.

Umaarufu wa Saanya uliongezeka zaidi baada ya kukataa bao la Simba lililofungwa na Ibrahim Ajib kwa madai kuwa aliotea, lakini akakubali bao la Yanga lenye utata ambalo lilifungwa na Amissi Tambwe ambaye inadaiwa aliunawa mpira kabla ya kufunga.

Na hapo ndipo kisa cha nahodha wa Simba, Jonas Mkude, kuonyeshwa kadi nyekundu kilipoanzia, ikidaiwa kuwa alijibizana na mwamuzi akipinga bao la Tambwe, hivyo kusababisha wacheze wakiwa pungufu uwanjani.

Katikati ya wiki iliyopita, Kamati ya Bodi ya Uendeshaji na Usimamizi wa Ligi Kuu, ilifuta adhabu ya kadi nyekundu ya Mkude kwa kutumia kanuni ya 9(8) ya ligi hiyo, baada ya kuthibitisha nahodha huyo hakuwa na makosa.

Kwa kutenguliwa adhabu hiyo ni wazi kwamba, Saanya alishindwa kuchezesha kwa kufuata sheria 17 za soka ikiwamo kuisababisha Simba kucheza pungufu uwanjani kwa makosa.

Kama mchezo ulichezeshwa kwa haki kwanini kamati ya bodi ya ligi itengue adhabu ya kadi nyekundu ya Mkude? Ni wazi kwamba bodi hiyo inatakiwa kuzama ndani zaidi ili kujionea makosa yaliyofanywa na waamuzi ambayo yamekichafua Chama cha Waamuzi Tanzania.

Kitendo cha kufutwa kwa adhabu ya kadi ya Mkude, kinapaswa kuwa somo kwa waamuzi wote wanaochezesha ligi mbalimbali zinazoendeshwa na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), kwani inaweza kuwa ni onyo kwa wengine.

Sasa ni wakati mwafaka kwa waamuzi kufuata sheria 17 za soka bila kufuata hisia zao kwenye mechi wanazochezesha.

Yote kwa yote, kiroho safi haina budi kusema kama kadi ya Mkude ni batili, basi Yanga walibebwa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
590,000SubscribersSubscribe

Latest Articles