24.9 C
Dar es Salaam
Wednesday, October 23, 2024

Contact us: [email protected]

Pluijm awaomba mashabiki Taifa

VAN-DERADAM MKWEPU NA WINFRIDA NGONYANI-DAR ES SALAAM

KOCHA Mkuu wa Yanga, Hans van Pluijm, amewaomba mashabiki wa timu hiyo kujitokeza kwa wingi katika mchezo wao wa marudio wa Kombe la Shirikisho Afrika dhidi ya Mo Bejaia ya Algeria, unaotarajiwa kuchezwa Jumamosi Uwanja wa Taifa Dar es Salaam.

Yanga itaingia uwanjani ikiwa na kumbukumbu ya kupoteza mchezo wa awali kwa kufungwa bao 1-0 dhidi ya wapinzani wao hao, katika mchezo wa kwanza wa Kundi A.

Akizungumza na MTANZANIA jana, Pluijm alisema ni wakati wa mashabiki wa timu hiyo kuendelea kuwasapoti na kuwaamini ili kuweza kufanya vizuri katika michezo yao iliyobakia ukiwamo wa Mo Bejaia.

“Kwani wiki hii wachezaji wameonekana kuwa na ari na hamasa ya kujituma uwanjani, inatupa faraja najua sitakuwa na mshambuliaji wangu, Donald Ngoma, aliyekuwa na kadi mbili za njano, Nadir Haroub (Cannavaro) kutokana na kuwa na majeruhi ya kifundo cha mguu lakini haitanifanya nikate tamaa,” alisema Pluijm.

Naye nahodha wa Yanga, Nadir Haroub ‘ Cannavaro’ , amesema watatengeneza ukuta imara ili kutoruhusu mabao katika mchezo wao wa kesho. Cannavaro aliliambia MTANZANIA jana kuwa beki ya Yanga ikiongozwa na yeye mwenyewe wataweka ukuta imara kuhakikisha washambuliaji wa Mo Bejaia hawaleti madhara.

“Moja ya safu ambazo kama hazijipangi vema zinaweza kuiletea madhara timu ni ngome ya ulinzi, sasa tutahakikisha kwamba hapiti mtu,” alisema Cannavaro. Naye mshambuliaji Mrundi, AmissiTambwe, ametamba kuwa lazima afunge katika mchezo huo baada ya kukosa bahati ya kufunga katika michezo iliyopita.

“Nimeshawasoma wapinzani tangu mchezo ule wa kwanza, hivyo nawatambua na kamwe hawatanibabaisha nitahakikisha napambana kufa au kupona,” alisema Tambwe. Mchezo huo utachezeshwa na waamuzi kutoka nchini Ethiopia ambapo mwamuzi wa kati atakuwa Bamlak Tessema Weyesa, akisaidiana na Kindie Mussioe na Temesgin Samuel Atango na mwamuzi wa akiba akiwa ni Haileyesus Bezezew Belete.

Viingilio vya mchezo huo vitakuwa ni Sh 3,000 kwa viti vya rangi ya kijani, bluu na chungwa, VIP B na C vikiwa ni Sh 10,000 huku VIP A ni Sh 15,000. Katika kundi hilo Yanga inashika mkia kwa kuwa na pointi moja, wakati mpinzani wake Mo Bejaia ikiwa nafasi ya pili kwa pointi sita, nafasi ya tatu Medeama ya Ghana yenye pointi nne huku kinara TP Mazembe ikiwa na pointi saba.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
590,000SubscribersSubscribe

Latest Articles