24.4 C
Dar es Salaam
Thursday, September 19, 2024

Contact us: [email protected]

Serikali kuimarisha sekta ya afya kwa mama na mtoto, Tanzania kuandaa mkutano wa 11 wa Merck Foundation

Na Esther Mnyika, Mtanzania Digital

Serikali ya Tanzania imeendelea kuwekeza katika sekta ya afya, hasa huduma za mama na mtoto, jambo lililoifanya nchi kuimarika katika utekelezaji wa malengo ya maendeleo ya kimataifa, yakiwemo Malengo ya Milenia na Maendeleo Endelevu (SDGs). Uwekezaji huu umeiwezesha Tanzania kuwa mwenyeji wa Mkutano wa 11 wa Taasisi ya Merck Foundation, utakaofanyika Oktoba 29-30, 2024.

Mkutano huo utafunguliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Samia Suluhu Hassan, na kuambatana na mkutano wa mabalozi wa nchi ambazo wake wa marais wao watashiriki. Kauli hii ilitolewa na Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dk. Dorothy Gwajima, leo Septemba 18, 2024, jijini Dar es Salaam wakati akitoa taarifa kuhusu maandalizi ya mkutano huo.

Dk. Gwajima alieleza kuwa kufanyika kwa mkutano huu nchini kunatokana na jitihada za Rais Dk. Samia katika kuwekeza kwenye sekta ya afya. “Merck Foundation ilipendekeza Tanzania kutokana na jitihada za wazi za serikali katika kuboresha afya ya mama na mtoto, na hii imesaidia taifa letu kufanya vizuri kwenye malengo ya kimataifa ya maendeleo,” alisema Dk. Gwajima.

Tanzania pia imechaguliwa kutokana na mazingira yake mazuri ya amani na utulivu, pamoja na uongozi bora wa Rais Samia, ambaye ameboresha diplomasia ya kimataifa. Mkutano huu utaratibiwa kwa ushirikiano kati ya serikali ya Tanzania na Taasisi ya Merck Foundation.

Merck Foundation na Lengo Lake

Merck Foundation ni taasisi ya uhisani yenye makao yake makuu Dubai, iliyoanzishwa mwaka 2017 kwa lengo la kuboresha upatikanaji wa huduma bora za afya na kujenga uwezo wa kisayansi katika jamii. Pia inalenga kuwawezesha wanawake na vijana katika nyanja za sayansi, teknolojia, uhandisi, na hisabati (STEM).

Mkutano huu wa kila mwaka unahusisha zaidi ya washiriki 6,000, wakiwemo watoa huduma za afya, watunga sera, wataalamu wa taaluma mbalimbali, na wanahabari kutoka zaidi ya nchi 70 za Afrika na Asia. Washiriki hunufaika na vikao vya kielimu na mafunzo kuhusu magonjwa mbalimbali kama kisukari, uzazi, saratani, na afya ya wanawake.

Washiriki na Mada za Mkutano

Mkutano wa mwaka huu unatarajiwa kuhudhuriwa na washiriki takriban 600, wakiwemo wake wa marais kutoka nchi za Afrika kama vile Angola, Botswana, Kenya, Ghana, na Liberia, huku Tanzania ikiwakilishwa na Mama Maria Mwinyi, mke wa Rais wa Zanzibar. Mawaziri wa Afya, Jinsia, Mawasiliano, Elimu, na Ustawi wa Jamii pia watahudhuria, pamoja na wataalamu wa afya na waandishi wa habari.

Mkutano huu utajadili mada nne kuu za kitaalamu: afya ya mama na mtoto, saratani, kisukari na shinikizo la damu, pamoja na mipango ya maendeleo. Aidha, utatoa fursa za mafunzo kwa vyombo vya habari vya afya, na kuweka mipango ya utekelezaji wa ahadi mpya zitakazotolewa na washiriki.

Faida za Mkutano kwa Tanzania

Dk. Gwajima alieleza kuwa mkutano huu utaongeza uelewa wa Watanzania kuhusu masuala ya afya, kuchangia malengo ya mkutano, na kuimarisha sifa za Tanzania kimataifa. Pia utaongeza pato la nchi kupitia sekta ya utalii, kwa kuwa washiriki watapata fursa ya kutembelea vivutio vya utalii nchini.

Kwa upande wake, Ofisa Mtendaji Mkuu wa Merck Foundation, Dk. Rasha Kelej, alisema mkutano huo utawezesha kubadilishana uzoefu kuhusu afya ya mama na mtoto, na kujenga kizazi cha usawa kwa nchi zitakazoshiriki.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
589,000SubscribersSubscribe

Latest Articles