24.5 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

27 zaidi wasimamishwa TRA

Pg 1*Watupwa korokoroni, polisi wawachunguza

*Bakhresa na wenzake waanza kulipa kodi

 

NA WAANDISHI WETU, DAR ES SALAAM

MAMLAKA ya Mapato Tanzania (TRA) wiki hii imewasimamisha kazi watumishi wake 27 wakituhumiwa kuhusika na upotevu na makontena 349 yaliyoisababishia Serikali hasara ya Sh bilioni 80.

Kusimamishwa kwa wafanyakazi hao kunafanya jumla ya waliosimamishwa kwa kashfa hiyo kufikia 35 huku uchunguzi zaidi ukiendelea kufanywa na makachero wa polisi.

Taarifa ya kusimamishwa kwa watumishi hao ilitolewa jana na Naibu Kamishna wa TRA, Dk. Philip Mpango, katika mkutano wake na waandishi wa habari uliofanyika ofisini kwake, Dar es Salaam.

Dk. Mpango, alisema watumishi 27 waliosimamishwa kazi wiki hii walikuwa wakifanya kazi katika geti namba tano na kwamba wanashikiliwa na Jeshi la Polisi kwa mahojiano na uchunguzi.

Alisema TRA inaendelea kupitia upya taratibu za utoaji wa leseni katika bandari kavu (ICDs) ili kuondoa mianya ya ukwepaji kodi pamoja na kuweka udhibiti wa uondoshaji mizigo kwenye bandari zote.

Dk. Mpango alisema ofisi yake imeanza kupanga upya safu ya watumishi wake ili kudhibiti upotevu wa kodi na kuondoa mianya ya uvujaji wa mapato.

Sambamba na hatua hiyo, Dk. Mpango alisema ofisi yake imebaini kampuni 43 zilizohusika na uingizaji wa makontena kinyume na taratibu.

Alizitaja kampuni hizo kuwa ni Lotai Steel Tanzania Ltd yenye makontena 100, Tuff Tyres Centre Company (58), Bin Slum Tyres Company Ltd (33), Tifo Global Mart (Tanzania) Company Limited (30), IPS Roofing Company Limited (20), Rushywheel Tyre Centre Co Ltd (12), Kiungani Trading Co Ltd (10) na Homing International Limited (9).

Kampuni nyingine alizozitaja ni Red East Building Materials Company Ltd (7), Tybat Trading Co Limited (5), Zing Ent Ltd (4), Juma Kassem Abdul (3), Salum Link Tyres (3), Ally Masoud Dama (2), Cla Tokyo Limited (2), Farid Abdullah Salem (2), Salum Continental Co (2), Zuleha Abbas Ali (2), Issa Ali Salim (2) na Snow Leopard Building (2).

Dk. Mpango alizitaja kampuni zilizokuwa na kontena moja kuwa ni Abdulaziz Mohamed Ally, Ahmed Saleh Tawred, Ali Amer, Ally Awes Alhamdany, Awadhi Salim Saleh, Fahed Abdallah Said, Hani Said, Hassan Husein Suleyman, Humud Suleiman Humud, Kamil Hussein Ali na Libas Fashion.

Nyingine ni Nassir Salehe Mazrui, Ngiloi Ulomi Enterprises Co. Ltd, Omar Hussein Badawy, Said Ahmad Hamdan, Said Ahmed Said, Salumu Peculier Tyres, Sapato N. Kyando, Simbo Yonah Kimaro, Strauss International Co. Ltd na Swaleh Mohamed Swaleh.

Alisema kampuni hizo zilipitisha makontena hayo katika bandari kavu (ICD) ya Azam inayomilikiwa na Said Salim Bakhresa and Company Limited iliyokuwa jumla na makontena 329.

Akizungumzia uchunguzi uliofanywa ili kubaini bidhaa zilizokuwa ndani ya makontena hayo, alisema ulibaini kuwa zilikuwa na matairi ya gari, samani mbalimbali, betri za gari, vifaa vya ujenzi, nguo na bidhaa nyingine mchanganyiko.

Alisema hatua inayofuata sasa ni kuhakikisha kampuni hizo zinalipa kodi inayostahili pamoja na kuwachukulia hatua watumishi wa TRA waliohusika kwenye kashfa hiyo.

Aidha, Dk. Mpango alisema tayari baadhi ya wafanyabiashara waliokwepa kulipa kodi wameanza kulipa sehemu ya kodi wanazodaiwa na hadi jana zilikuwa zimelipwa Sh bilioni 5.2.

“Kwa mujibu wa maagizo ya Rais John Magufuli, tunawataka wahusika wengine wajitokeze kulipa kodi ndani ya siku hizi za huruma alizowapa kwa sababu zikiisha sheria stahiki zitachukuliwa dhidi yao,” alisema Dk. Mpango.

Aliwataja baadhi ya walioanza kulipa kodi waliyokwepa kuwa ni Said Salim Bakhresa and Company Limited Sh bilioni 2.17, Tuff Tyres Center Co Ltd Sh bilioni moja, Kiungani Trading Co. Ltd Sh 506,728,362.70 na Binslum Tyres Co. Ltd ambaye awali alilipa Sh bilioni 1.4 kabla ya kumalizia deni lake kwa kulipa Sh bilioni 1.15

“Mchana huu (jana) tunatarajia Bakhresa atalipa Sh bilioni 2 nyingine ambazo ni sehemu ya deni la kodi anayodaiwa,” alisema Dk. Mpango.

Wakati huo huo watuhumiwa saba wa utoroshaji makontena 349 katika bandari ya Dar es Salaam ulioisababishia Serikali hasara ya Sh bilioni 80 jana walifikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.

Washtakiwa hao walifikishwa mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakama ya Kisutu, Huruma Shaidi na kusomewa mashtaka mawili kila mmoja na Wakili Mkuu wa Serikali, Timos Vitalis, akisaidiana na Wakili wa Serikali Mwandamizi, Christopher Msigwa.

Alidai shtaka la kwanza likiwa la kula njama ya kudanganya Serikali kuwa makontena yaliyokamatwa bandarini na kupelekwa katika bandari kavu ya Azam yalikuwa yamelipiwa kodi zote.

Alidai shtaka la pili linalowakabili washtakiwa hao kwa pamoja waliisababishia Serikali hasara ya Sh bilioni 80 kwa kuinyima TRA kukusanya kodi jambo ambalo ni kosa kwa mujibu wa aya ya 10 kifungu kidogo cha kwanza cha sheria ya uhujumu uchumi, sura ya 200 iliyorejelewa 2002.

Alidai katika shtaka la pili washtakiwa kwa pamoja wanadaiwa kuwa kati ya Juni mosi na Novemba 17, mwaka huu katika Mkoa wa Dar es Salaam walishindwa kutimiza majukumu yao na kusababishia Serikali hasara.

Washtakiwa hao ni pamoja na Kamishna wa Idara ya Forodha na Ushuru wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Tiagi Masamaki (56), Meneja Kitengo cha Huduma za Ushuru, Habib Hamis (45), Meneja Udhibiti na Utekelezaji, Button Mponezya (51), Msimamizi wa Kitengo cha Mawasiliano na Kompyuta (Azam), Eliaichi Mrema (31), Msimamizi Kitengo cha Mawasiliano ya Kompyuta  (TRA), Hamis Omary (48), Mchambuzi Mwandamizi wa Masuala ya Biashara Haroun Mpande (48) na Meneja wa Azam, Ashraf Yusuph (59).

Washtakiwa hao walirudishwa rumande baada ya kukosa dhamana hadi kesi yao itakapotajwa tena Desemba 17, mwaka huu.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles