24.4 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 23, 2024

Contact us: [email protected]

Wiki ya madini, wachimbaji zaidi ya 2,000 kukutana Mwanza

Na Clara Matimo, Mwanza

Wachimbaji wadogo wa madini zaidi ya 2,000  kutoka mikoa mbalimbali nchini wanatarajia kukutana Mei 3 hadi 10, mwaka huu 2023 jijini Mwanza kuadhimisha wiki ya madini kitaifa na kongamano la wachimbaji wa madini Tanzania ambao watazungumzia masuala ya uchimbaji.

Pia wachimbaji hao watahudhuria mkutano Mkuu wa Shirikisho la Vyama vya Wachimbaji Wadogo wa Madini Tanzania(FEMATA) utakaofanyika Mei 10, katika ukumbi wa Rock City Mall jijini hapa.

Katibu Mkuu Kamati ya Kitaifa ya Maandalizi ya Mkutano Mkuu wa Femata, Kongamano la wachimbaji Madini na Wiki ya Madini mwaka 2023, Solomon Mabati akizungumza na mwandishi wa habari hii (hayupo pichani).

Hayo yameelezwa na Mkurugenzi wa Habari wa FEMATA Dk. Benard Joseph, Aprili 21, 2023  alipozungumza na Mtanzania ofisini kwake kuhusu maandalizi ya wiki ya madini na kongamano hilo ambalo kitaifa litafanyika jijini Mwanza kwenye viwanja vya Rock City Mall.

 “Maandalizi yanakwenda vizuri kabisa, kongamano  hilo  litawakutanisha wadau mbalimbali wa sekta ya madini kutoka ndani na nje ya nchi litaambatana na mambo tofautitofauti ikiwemo maonesho ya teknolojia za kisasa za uchimbaji madini, elimu ya mikopo ya uchimbaji kutoka taasisi za fedha na elimu ya afya kwa ajili ya kutunza afya na mazingira kwenye nchi yetu.  

“Kongamano la wachimbaji litafanyika Mei 9, 2023 ambapo tunatarajia kupata mgeni rasmi kiongozi wa kitaifa, litafuatiwa na usiku wa madini pale viwanja vya Hotel ya Malaika ambao utaambatana na kutoa tuzo za aina mbalimbali  kwa watu walioshirikiana vyema na FEMATA katika kufanikisha shughuli za uchimbaji na waliolipa tozo na kodi zao vizuri,”alisem Dk. Joseph na kuongeza

“Sasa hivi wachimbaji tunakaribia kufikia asilimia 10 kwenye kuchangia pato la taifa kwa hiyo tunatembea kifua mbele kwa ajili ya mafanikio hayo na tumeona itapendeza sana tukiwapa tuzo wadau waliofanikisha hilo,”alisema Mkurugenzi huyo wa Habari kutoka FEMATA.

Katibu Mkuu Kamati ya Kitaifa ya Maandalizi ya Mkutano Mkuu wa FEMATA, Kongamano la Wachimbaji na Wiki ya Madini 2023, Solomon Mabati alisema faida ya mkutano huo na mingine ya namna hiyo iliyokwishafanyika miaka ya nyuma ni kuwawezesha wachimbaji kuwasilisha serikalini changamoto zao kwa utaratibu mzuri bila namna yoyote ya uharakati na serikali kuzitafutia ufumbuzi.

Aidha Mabati aliipongeza serikali  kwa kusikiliza changamto za wachimbaji na kuzitafutia ufumbuzi kwani miaka saba iliyopita walikuwa wakikabiliwa  na uhaba wa maeneo ya uchimbaji  na wachimbaji wadogo walikuwa wanaitwa wachimbaji haramu sasa wamelasimishiwa,  ukosefu wa masoko ya kuuzia madini ambapo uwepo wa masoko umesaidia udhibiti wa masoko nchini  na ukosefu wa mitaji unaotokana na taasisi za fedha bado hazijaamini sana kwenye uchimbaji.

“Zaidi ya asilimia 95 ya wachimbaji wadogo wa madini nchini wanakabiliwa na changamoto ya ukosefu wa mitaji kwa sababu taasisi za fedha bado hazijaamini sana kwenye uchimbaji lakini kwa sababu serikali imetulasimishia sisi wachimbaji  maeneo ya kuchimba imetusaidia maana tunakopeshana na kudhaminiana wenyewe kwa sababu hatuna hofu,”amesema Mabati.

Mabati aliiomba serikali kupitia kauli mbiu ya maadhhimisho hayo kitaifa mwaka huu 2023 isemayo  ‘Amani iliyopo Tanzania Itumike Kuwa Fursa ya Kiuchumi na Tanzania Kuwa Kitovu cha Biashara ya Madini Afrika’ kuona namna gani ya kuifanya nchi kuwa  kitovu cha madini kupitia amani iliyopo ili kuinua zaidi uchumi wa taifa na wananchi wake.

“Tukifauru kuiwezesha Tanzania kuwa kitovu cha madini katika bara la Afrika tutakuwa na watu wengi zaidi ya 1000 wanaoingia kununua na kuuza madini nchini kwetu hivyo  tutapata faida mbalimbali ikiwemo biashara zingine kufanyika kwa kiwango kikubwa.

 “Maana wanaoleta madini nchini na wanaokuja kununua watalala kwenye hotel za Tanzania, watanunua bidhaa katika maduka yaliyopo nchini na watafanya utalii kwa hiyo uchumi wetu utakuwa zaidi,”alishauri Mabati.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles