25.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

Wenye nyumba kuisoma namba

Dk. Philip Mpango

Na Waandishi Wetu, Dar es Salaam

SERIKALI inatarajia kuwasilisha muswada mpya wa Sheria ya Fedha ya Mwaka 2016 bungeni unaotajwa kuwa utawabana na kuwakamua watu mbalimbali wakiwamo wafanyabiashara na wamiliki wa nyumba.

Muswada huo unaotarajiwa kuwasilishwa kwa mara ya pili bungeni wiki ijayo, unakuja baada ya Juni 8, mwaka huu, Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Philip Mpango, kusoma bungeni bajeti kuu ya Serikali ambayo wabunge pamoja na wabobezi wa masuala ya uchumi walisema itawaumiza makabwela kutokana na watu wa tabaka la juu na kati kubanwa.

Taarifa za uhakika ambazo MTANZANIA Jumapili imezipata kutoka kwa vyanzo vyake mjini Dodoma jana, zilisema muswada huo uliowasilishwa kwa mara ya kwanza bungeni Juni 10, mwaka huu na kuwekwa hadharani Juni 13, unazua hofu hasa kwa wafanyabiashara huku ukiwataka wenye nyumba kulipa kodi kutoka katika fedha wanazolipwa na wapangaji wao.

Chanzo kimoja kilisema kuwa katika moja ya mabadiliko ya vifungu vya muswada huo, Kamishina Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) atapitia mkataba wa kodi wa mwenye nyumba na mpangaji na atatangaza gharama za upangishaji katika Gazeti la Serikali.

“Rais John Magufuli ameamua kukusanya kodi katika maeneo ambayo zamani yalikuwa hayakusanywi na lengo lake ni kuongeza mapato ya Serikali kupitia vyanzo vipya. Ndiyo maana kuna muswada unapelekwa bungeni ili sheria za zamani za fedha zifanyiwe marekebisho,” kilisema chanzo hicho na kuongeza:

“Marekebisho ya sheria hiyo yatakuwa katika maeneo mbalimbali na huenda yakabadilisha kabisa mwenendo wa biashara na shughuli mbalimbali zinazofanyika hapa nchini.

“Kifungu cha 8 cha sheria kimebadilishwa na sasa katika muswada huu mpya kitamtaka Kamishina Mkuu wa TRA kufanya utafiti kuhusu eneo husika kabla ya kuanza kutoza kodi na kila eneo litakuwa na gharama zake, hivyo itakuwa ni vigumu kukwepa au kudanganya.”

Mbali na hayo, pia chanzo kingine kililiambia MTANZANIA Jumapili kuwa kama mtu atapinga kadirio la kodi, muswada huo utamtaka alipe kwanza kwa asilimia 100 ndipo apinge katika Mahakama ya Kodi.

Kiliendelea kusema kuwa muswada huo uliosainiwa Mei 26, mwaka huu na Dk. Mpango, unasema kuna faini ya asilimia tano kwa kila mwezi kwa mtu atakayechelewa kulipa kodi.

“Kamishina Mkuu wa TRA kapewa mamlaka makubwa na yenye kuumiza, mathalani muswada huo utampa mamlaka ya kumlazimisha mtu kulipa kodi bila kumfikisha mahakamani,” kilisema.

Pia muswada huo unataka kila kodi au mapato ya Serikali yatakayokusanywa yapelekwe Serikali Kuu ili kuyadhibiti yasipotee.

“Kifungu cha 5 cha muswada huo wa sheria ya fedha kimefanyiwa marekebisho  na sasa kinasema kila kodi au mapato yatakwenda Serikali Kuu,” kilisema chanzo hicho.

Kwamba muswada huo utamtaka Waziri wa Fedha baada ya kushauriana na Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) ndipo atoze kodi kutokana na eneo husika na kutangazwa katika Gazeti la Serikali.

“Muswada huo pia umebadilisha kifungu cha 16 cha sheria ya fedha na kitamtaka Waziri wa Fedha kushauriana na mwenzake wa Tamisemi kabla ya kuanza kutoza kodi katika eneo husika,” kilisema chanzo hicho.

Kiliendelea kusema kuwa baadhi ya wabunge, Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti na Wizara ya Fedha na Mipango wamekuwa wakikutana na kufanya vikao vya kuchambua vipengele mbalimbali vya muswada huo kabla haujawasilishwa.

Alipotafutwa Dk. Mpango jana ili atoe ufafanuzi wa vipengele vinavyotajwa kuwa vitakuja kuwabana wafanyabiashara na kuwakamua wenye nyumba, simu yake ya mkononi ilikuwa haipatikani.

Naye Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Ashatu Kijaji alipotafutwa, hakupokea simu alipopigiwa na hata alipotumiwa maswali kwa ujumbe mfupi wa maandishi (sms) hakujibu, huku Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti ambaye aliwahi kuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Tamisemi), Hawa Ghasia, pia simu yake ya mkononi ilikuwa haipatikani.

Akizungumzia muswada huo, mbobezi wa uchumi kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Profesa Haji Semboja,   alisema Serikali inapaswa kutekeleza muswada huo kwa uangalifu ili kuondoa malalamiko kwa jamii.

Alisema sheria ya kukusanya mapato haina shida kama inaingiza kipato kwa Serikali  kutokana na nguvu ya mwananchi au chombo kinachopaswa kukatwa kodi.

“Sidhani kama Serikali hawakuwa na ufahamu na vipengele vya kodi vinavyotajwa kuwa vitawaumiza watu, naamini zipo kodi nyingi za mapato katika ardhi na matumizi ya ardhi, lakini kama wameamua kudai kodi za wapangaji inabidi wawe waangalifu.

“Watanzania wengi wenye nyumba ni masikini na nyumba zipo za aina nyingi kulingana na thamani, sio kila  inayopangishwa inaweza kuwa na uwezo  kulipa kodi,” alisema Profesa Semboja.

Pia alisema malipo ya kodi lazima yaangaliwe na maeneo husika kwa kufanya utafiti kupitia kwa wenye nyumba wenyewe.

“Watu wanaangalia nyumba za kupanga, lakini wanapaswa kujua wapangaji wanaofanya biashara mfano za fremu wanahangaika hadi kupata kodi na kusumbua wenye nyumba, wasiwasi wangu mkubwa kunaweza kukatokea tatizo la kubambikiziana kodi, kuoneana na kuzua mianya ya rushwa kwa wakusanya mapato katika maeneo husika,” alisema.

Profesa Semboja alisema Serikali kupitia TRA haitakiwi kukurupuka kutekeleza muswada huo badala yake itoe elimu na taratibu zitakazotumika ili kuwa na mfumo mzuri wa kukusanya mapato hayo.

Alisema Serikali inapaswa kuwa na chombo cha kuangalia na kusimamia faida na hasara zitokanazo na ukusanyaji wa mapato katika baadhi ya vyanzo, zikiwemo nyumba za kupanga.

Kuhusu utaratibu wa kila kodi na mapato ya Serikali kuingia moja kwa moja mfuko wa Serikali Kuu, alisema wahusika hawapaswi kukurupuka kuchukua kila kodi kuilekeza huko kwa kuwa kuna aina nne za kodi ambazo kila moja ina kazi yake.

“Kuna haja ya kujua tofauti ya kila kodi na matumizi yake, mfano kuna kodi ambazo zinapaswa zitolewe ili zisaidie wakazi wa maeneo husika, sasa kodi za hivyo zikienda serikalini wananchi watapata wapi huduma zao? Kwa hiyo hili suala linapaswa liangaliwe kwa undani, tunajua Serikali inatafuta fedha, lakini umakini unahitajika,” alisema.

Profesa Semboja alisema inapaswa kutambua sehemu wanazopaswa kukusanya kodi na kuzielekeza moja kwa moja serikalini ili wasiharibu na kuingilia utaratibu wa watu wengine kukusanya mapato kupitia vyanzo vyao.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles