25.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Walioua mifugo kwa chanjo wasakwa

Na Edward Kondela

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mashimba Ndaki, ameagiza kusakwa kwa wataalamu wa mifugo waliotoa chanjo ya mifugo katika Kijiji cha Mlazo Wilaya ya Chamwino, mkoani Dodoma, na kusababisha baadhi kufa na mingine kupata madhara, kufikishwa kwa Baraza la Veterinari Tanzania kwa uchunguzi.

Waziri Ndaki  amesema hayo jana alipofika katika kijiji hicho baada ya kupatiwa taarifa juu ya madhara yaliyojitokeza  kwa mifugo hiyo iliyopatiwa chanjo ya Homa ya Mapafu (CBPP).

Mifugo ilikufa ni ng’ombe 25, 33 mimba zikitoa na 58 kuvimba sehemu waliyochomwa sindano, kwa upande wa mbuzi alikufa mmoja, waliovimba watano, waliotoa mimba 12 na upande wa kondoo waliokufa 20, waliovimba 16 na waliotoa mimba watano.

Kutokana na hali hiyo, Ndaki amesema zoezi la chanjo ya mifugo dhidi ya magonjwa linaloendelea nchini lina lengo zuri, lakini amesikitishwa na kilichofanyika katika kijiji  hicho sababu  haikufanyika kwa kuzingatia kanuni za kitaalamu na kuagiza pia Kampuni ya Agristeps Limited iliyoingia mkataba na Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino kusimamia zoezi la utoaji chanjo, kuzuiwa kuendelea.

“Wale wataalamu waliochanja ng’ombe wa hawa wafugaji, watafutwe majina yao, wamesomea wapi, wapelekwe kwa Msajili wa Baraza la Veterinari Tanzania hatuwezi kuendelea kuua ng’ombe namna hii.

“Hii  kampuni ilitakiwa ijiridhishe na utaratibu na mchakato mzima wa uchomaji wa chanjo kwa kuwa amefanya kazi hii kuwa mbovu, asimame kuendelea kutoa chanjo kwenye Wilaya ya Chamwino tafuteni mwingine,” ameagiza Ndaki.

Kuhusu mifugo inayopata madhara wakati wa utoaji chanjo kutokana na sababu mbalimbali, amesema kuna haja ya kubadilisha Sheria ya Veterinari ya mwaka 2003 na Sheria ya Magonjwa ya Wanyama ya ili endapo mifugo ikipata madhara yoyote mfugaji aweze kufidiwa mifugo hiyo.

Naye Mkurugenzi wa huduma za mifugo kutoka wizarani Prof. Hezron Nonga amesema uchunguzi uliofanywa umebaini kuwa sindano zilizotumika zilikuwa ndefu na kwamba mifugo ilipaswa kuchomwa chini ya ngozi maeneo ya shingoni ambapo kuna ngozi nene na siyo kwenye mguu ambapo ngozi yake ni nyembamba kwa kuwa chanjo hiyo haipaswi kugusa nyama.

Prof. Nonga amefafanua kuwa chanjo hiyo imeelekeza kuwa endapo ikiingia ndani ya nyama inasababisha nyama kuharibika kwa kuwa inaua seli za mwili kama ambavyo imefanyika kwa baadhi ya mifugo kupata uvimbe, majipu na usaha maeneo ambayo imechomwa chanjo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles