NA AZIZA MASOUD, DAR ES SALAAM
MAMLAKA ya Mapato nchini (TRA) imekusanya Sh bilioni 10.75 kati ya Sh bilioni 80 zinazodaiwa kutoka kwa wafanyabiashara waliokwepa kodi kwa kupitisha makontena 329 bila kulipa ushuru.
Fedha hizo zimekusanywa ndani ya siku sita baada ya Rais John Magufuli kukutana na wafanyabiashara Ikulu jijini Dar es Salaam na kuwapa siku saba kulipa fedha hizo kabla ya kuchukuliwa hatua za kisheria.
Akizungumza na MTANZANIA Jumamosi, Mkurugenzi wa Huduma na Elimu kwa Mlipa Kodi wa TRA, Richard Kayombo, alisema fedha hizo zimekusanywa kutoka kwa wafanyabiashara 22 kati 43 wanaomiliki makontena hayo.
“Bado wanaendelea kulipa, siku saba alizotoa Rais Magufuli zinaisha kesho (leo) lakini mpaka sasa tumekusanya Sh bilioni 10.75 kutoka kwa waagizaji 22,” alisema Kayombo.
Alisema baada ya muda uliotolewa na Rais Magufuli kwisha taratibu nyingine za kisheria zitafuata ili kuweza kuhakikisha wahusika wanawajibika kwa makosa yao.
Novemba 23, mwaka huu, Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, alifanya ziara ya kushtukiza TRA na kubaini upotevu wa makontena 329 yaliyokuwa yakidaiwa kodi ya Sh bilioni 80.
Sakata hilo lilisababisha kusimamishwa kazi kwa Kamishna Mkuu wa TRA, Rished Bade pamoja na watumishi wengine wanane akiwemo aliyekuwa Kamishna wa Forodha, Tiagi Masamaki.