25 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

Wakulima wa pamba Igunga waomba kupunguziwa tozo

Na Allan Vicent, Igunga

WAKULIMA wa zao la pamba wilayani Igunga mkoani Tabora, wameomba Serikali iwasaidie kuondoa au kupunguza tozo za kodi wanazokatwa wakati wa maandalizi ya masoko ya zao hilo ili wanufaike zaidi.          

Wametoa kilio hicho jana kwenye mahojiano maalumu na Mtanzania Digital,alipotembelea Amcos hiyo ili kujionea hali ya maisha ya wakulima na maendeleo yao katika zao hilo na changamoto zinazokabili.

Mkulima Olingo Sombe ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chama cha Msingi Igunga Balimi AMCOS, aliishukuru Serikali kwa kuwarahisishia upatikanaji wa pembejeo kwa wakati ila akalalamikia wingi wa tozo wakati wa mauzo ya zao hilo.

Amesema katika msimu uliopita wa 2020/2021walifanya vizuri sana ambapo kwa zao la pamba walivuna jumla ya kilo 200,000 na choroko kilo 700,000 na waliuza kwa bei nzuri iliyowaongezea mapato ila tozo zilichangia kupunguza mapato yao.

Ametaja tozo hizo kuwa ni gharama ya kupakia ambapo kila gunia wanakatwa sh 300 kwa kila mkulima, kushindilia ujazo wa gunia wanakatwa sh 300 na kusindikiza gari kupeleka mzigo kwa kampuni wanakatwa sh 50,000 ili kumlipa mhusika.  

‘Haya makato yanatuumiza, tumeshafikisha kilio chetu kwa viongozi mbalimbali akiwamo Ofisa Ushirika, Mkuu wa Wilaya na juzi tumemweleza Balozi wa pamba nchini Aggrey Mwanri ili waangalie namna ya kutusaidia’, amesema.

Adelina Braz ambaye pia ni mkulima wa pamba na choroko wilayani humo, amesema tozo hizo ni kilio chao cha muda mrefu ambacho hakijatatuliwa, anaamini zitapunguzwa  na wakulima wengi watanufaika na zao hilo.

Ameomba gharama ya kupakia na kusindikiza mzigo ilipwe na kampuni husika kama ilivyokuwa zamani wao walipe gharama ya kushindilia tu ili kuwapunguzia mzigo wa makato.

Aidha ameshauri kila kampuni kubeba mzigo wake punde wanaponunua ili kuepusha gharama za usindikizaji.

Akitolea ufafanuzi malalamiko hayo, Kaimu Meneja Mkuu wa Chama Cha Ushirika wa Wakulima wa Pamba Mkoani hapa (Igembensabo) Juma Mrisho,amesema tozo hizo ni makubaliano yaliyofikiwa katika kikao cha pamoja baina ya wakulima na wadau wa pamba kutegemeana na bei ya soko.

Ameongeza kuwa gharama za tozo hizo zipo kwenye mkokotoo wa bei kulingana na soko la dunia hivyo haziwezi kuondolewa mara moja hadi vikao vya pamoja vikae na kuafikiana.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles