23.4 C
Dar es Salaam
Saturday, April 27, 2024

Contact us: [email protected]

Wajasiriamali 680 wapewa mafunzo Mwanza

Na Clara Matimo, Mwanza

Watu zaidi ya 680 wenye ndoto ya kuwa Wajasiriamali wanaoishi jjijini Mwanza wamepewa mafunzo jinsi ya kutengeneza bidhaa za viwandani kwa njia rahisi, kilimo, ufugaji mapishi na usindikaji wa matunda ili waweze kujiajiri wajiingizie kipato wao na serikali.

Mafunzo hayo ya siku tatu yaliyofanyika hivi karibuni jijini hapa yametolewa bila malipo na kampuni ya Academician Multisolution inajojishughulisha kudhamini , kusimamia, kutoa mafunzo na kuwajengea uwezo wasanii na wajasiriamali ili kuboresha maisha ya mtanzania mwenye kipato duni kwa kushirikiana na Mjasiriamali Kwanza Industry.

Akizungumza wakati akitoa mafunzo hayo kwa wajasiriamali hao, Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni ya Academician Multisolution, Dk. Emmanuel Nyagabona, aliwasihi washiriki wote kutumia ujuzi walioupata ili waweze kujiajiri na kujiingizia kipato kwani malighafi zote za kutengeneza  bidhaa walizofundishwa zinapatikana jijini Mwanza.

“Tumewapa mafunzo haya bure  ili yakawe chachu katika kukuza kipato chenu binafsi, familia zenu na taifa kwa jumla, tutaendelea kuwafuatilia ili tujue kila mmoja wenu anatengeneza bidhaa ipi kati ya mlizojifunza lengo letu ni kuona wote mmejiajiri,”alisema Dk. Nyagabona.

Kwa upande wake Mkurugenzi idara ya mafunzo kutoka kampuni hiyo, Sharifa Banana, alisema wametoa  elimu hiyo bure maana walilenga kutoa huduma kwa jamii  kulingana na changamoto ya ukosefu wa ajira na uelewa namna ya kusajili vikundi, jinsi ya kuandika andiko mradi ili wapate  mikopo kutoka taasisi mbalimbali za fedha pamoja na ile inayotolewa na serikali kupitia halmashauri itakayowasaidia kupata mitaji.

Sharifa aliiomba serikali kutenga eneo maalum  kwa ajili ya wajasiriamali ili wawe sehemu moja kwani itasaidia kuwa na ushindani wa kutengeneza bidhaa  zenye ubora pamoja na bei.

 “Serikali yetu ni sikivu na inajali sana wananchi wake ndiyo maana inatenga asilimia 10 ya mapato kwenye kila halmashauri kwa ajili ya kutoa mikopo kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu, mikopo hiyo inatunufaisha  na sisi wajasiriamali hivyo tunaomba itusaidie kutujengea jengo ambalo kila mjasiriamali akiisha tengeneza bidhaa zake atapeleka hapo kama ilivyo machinga complex ya jijini Dar es Salaam na sisi tujengewe wajasiriamali compex,”alisema.

Mratibu wa mafunzo hayo, Edwin Kabide, alisema lengo lao ni kuwafikia wajasiriamali 5,000 hadi 10,000 baada ya miaka mitano hadi sita kutoka mikoa mbalimbali nchini kwani hadi sasa wameishapokea maombi kutoka kwa wakazi wa mikoa  na wilaya tofauti tofauti wakiwaomba waende wakawape elimu hiyo maana wanauhitaji ikiwemo  Kilimanjaro, Ukerewe na Magu za mkoani Mwanza.

“Naomba nitumie fursa hii kuwatoa hofu wakazi wa mikoa na wilaya zote ambao wametupigia simu na kutuomba tufike kwenye maeneo yao kuwapa mafunzo  kama tuliyoyatoa jijini hapa, Mwenyezi Mungu akituwezesha tutawafikia  maana mafunzo yetu ni endelevu pia yako tofauti na ambayo wengine wanayatoa kwanza huwa wanawatoza  washiriki fedha lakini sisi tunayatoa bure.

 “Kila watu ambao  tunawapa mafunzo tunawaingiza kwenye data base, tunawapa vyeti pia sisi ni daraja baina yao na serikali maana taarifa zao ambazo tunazihifadhi zitaisaidia serikali kuwatambua hivyo itakuwa rahisi  kuwapa mikopo kwa ambao hawana mitaji na walio nayo wataendelea kufanya biashara lakini wataendelea kuboreshewa mazingira maana wanatambulika kwa idadi,”alisema Kabide.

Kwa mujibu wa Kabide walitarajia kutoa mafunzo hayo kwa watu 500 wa wilaya ya Ilemela lakini jumla ya washiriki walikuwa 700 kutoka wilaya hiyo, Nyamagana na baadhi walitoka mkoa wa Mara.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles