Neema Paul, TUDARCO
Katibu Mkuu wa Umoja wa Vijana CCM Tanzania(UVCCM), Kenan Kihongosi ameagiza kuchukuliwa hatua za kiutendaji wahudumu wa kituo cha afya cha Kijiji cha Mbika, kilichopo jimbo la Ushetu Wilaya ya Kahama, mkoani Shinyanga baada ya kuwepo kwa malalamiko kutoka kwa wananchi juu ya utoaji huduma usioridhisha.
Kihongosi amezungumza hayo katika uzinduzi wa kampeni za uchaguzi mdogo wa jimbo hilo baada ya kufariki kwa aliyekua mbunge wake Elias Kwandikwa ambapo ametaka kupata maelezo kutoka kwa mganga mkuu wa halmashauri kwa nini dawa hazipatikani katika kituo hicho hadi wakanunue maduka ya nje yanayomilikiwa na wahudumu hao.
Amesema pia wahudumu wa kituo hicho cha afya wanatoa lugha chafu kwa wagonjwa wanapokwenda kupata matibabu.
“Wagonjwa wakija hapa mnawatukana ,mnawafokea mnasahau kuwa wao ndio serikali na sisi tupo hapa kwa ajili ya kuwahudumia wao hii si haki,” amesema.
Aidha Kihongosi ametoa onyo kwa tabia ya baadhi ya wauguzi kuacha tabia ya kuchukua dawa hospitalini hapo na kuzipeleka kwenye maduka yao binasfi kwani kufanya hivyo ni kuwaumiza wananchi wenyewe na kutoa maagizo kwa Emmanuel Cherehani ambaye ni mgombea ubunge katika jimbo hilo kupitia tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuacha kufumbia macho suala hilo na kuwawajibisha wale wote wanaohusika
“Unaenda hospital unaambiwa dawa hakuna lakini nenda duka fulani utapata hiyo dawa sasa hii si sawa? amehoji katibu huyo.
Naye Mjumbe wa Halmashauri Kuu CCM-Vijana, Mussa Mwakitinya ametoa rai kwa wananchi wa Mbika kuchagua kiongozi bora ambaye anaweza kusimama na kuwawakilisha bungeni.