24.2 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 16, 2024

Contact us: [email protected]

WAANDISHI WAMTANGAZIA MGOMO DC KIBAHA

NA GUSTAPHU HAULE-PWANI


 

assumpter-mshamaCHAMA cha Waandishi wa Habari Mkoa wa Pwani (CRPC) kimetangaza mgomo wa kususia kufanyakazi za Mkuu wa Wilaya ya Kibaha, Assumpter Mshama kutokana na kitendo chake cha kumdhalilisha mwandishi wa habari wa gazeti la Mwananchi, Sanjito Msafiri.

Chama hicho pia kimetoa siku saba kwa mkuu huyo wa wilaya kumwomba radhi mwandishi huyo kinyume na hapo hakuna mwandishi yeyote atakayeshiriki ama kuandika shughuli yoyote inayomuhusu kiongozi huyo.

Mwenyekiti wa CRPC, Mkoa wa Pwani Ally Hengo alisema Novemba 29 mwaka huu Gazeti la Mwananchi lilitoa habari iliyoelezea namna Kibaha Mjini walivyopuuza agizo la Rais Dk. John Magufuli la kufanya usafi kila Jumamosi ya mwisho wa mwezi.

Hengo alisema kuwa baada ya habari hiyo kutoka kwenye gazeti hilo,  asubuhi yake  Mshama alimpigia simu mwandishi huyo akimshutumu juu ya taarifa hiyo.

Alisema ilipofika saa tano siku hiyo, Katibu Tawala wa Wilaya ya Kibaha (DAS), Sozi Ngate naye alimpigia simu kwa mara ya pili mwandishi huyo na kumwarifu ahudhurie mkutano wa wafanyabiashara uliotarajiwa kufanyika saa nane mchana.

“Baada ya kufika katika mkutano huo alimkuta mkuu wa wilaya, wafanyabiashara na viongozi wengine wa serikali ambapo Mshama alimwamuru mwandishi kusimama mbele ya watu ili asome kile alichokiandika huku akimtolea lugha za kejeli,”alisema Hengo.

Aidha Mshama aliendelea kumsuta mwandishi huyo mbele ya watu kwa madai kuwa habari yake inamchonganisha na Rais Dk. Magufuli na kwamba lazima amwombe radhi mbele ya watu hao.

Alisema pamoja na amri za kushurutishwa zilizokuwa zinatolewa na mkuu huyo mwandishi aligoma kuisoma habari hiyo mbele ya watu kwa madai kuwa alichokiandika ni ukweli kwakuwa uchafu uliopo Kibaha ni mkubwa.“Kutokana na tukio hilo uongozi  na wanachama wa klabu ya waandishi wa habari Mkoa wa Pwani umekutana na kulaani kitendo hicho na kumtaka mkuu wa wilaya kuomba radhi kwa mwandishi huyo kwa udhalilishaji huo alioufanya,”alisema Hengo.

Aidha chama hicho pia kimemtaka mwenyekiti wa Soko la Mailimoja Ramadhani Maulid kumwomba radhi kwa kumshurutisha mwandishi huyo kupiga magoti mbele ya hadhara hiyo.

Akizungumzia kadhia hiyo aliyoipata, Msafiri alisema hakuwa amevunja sheria yoyote katika maandishi yake kwa sababu aliifanyia uchunguzi habari hiyo na kubaini kuwepo kwa uchafu mkubwa katika Mji wa Kibaha.

Hivyo agizo la Rais Dk. Magufuli la kufanya usafi kila Jumamosi ya kila mwisho wa mwezi halikutekelezwa.

Alisema kuwa, siku ya Jumamosi inapofika wafanyabiashara waliopo Mjini Kibaha wamekuwa wakifunga maduka yao na kuyafungua muda wa saa nne kwa ajili ya kukwepa faini ya Sh 50,000 na kwamba hakuna usafi wanaofanya.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles