Sheila Katikula, Mwanza.
Afisa Ustawi wa Jamii Halmashauri ya Wilaya ya Ilemela, Stella Mbura ametoa wito kwa waajiri kujenga tabia ya kutoa mikataba ya kazi kwa wafanyakazi wa majumbani ili kuwezesha kila mmoja kutimiza majukumu yake.
Stella ametoa wito huo alipokuwa akizungumuza katika warsha ya waajiri na wafanyakazi wa majumbani iliyoandaliwa na Shirika lisilokuwa la kiserikali la Women Action on Ecohealth and Legal Rights.
Alisema imefikia wakati sasa kwa jamii kutambua umuhimu wa kutoa mikataba kati ya mwajiri na mfanyakazi ili kuepuka malalamiko na migogoro ambayo hujitokeza wakati kipindi chote cha kazi.
Alieleza kupitia shirika hilo linalojishughulisha na kuelimisha wanawake na watoto kujua haki na wajibu wao kulingana na sheria za nchi basi ni vyema jamii ielimishwe juu ya haki za waajiri na haki za wafanyakazi ikiwemo mikataba.
Aidha alihimiza suala la umri kuangaliwa zaidi kwani wafanyakazi wenye umri kati ya miaka 14- 17 bado wana hitaji malezi na wanachangamoto za kupevuka hivo ni bora kuajiri watu wazima.
Hata hivyo amewataka waajiri hao kuishi na wafanyakazi wa nyumbani kama watoto wao kwa kuwathamini,kuwapenda na kuwalinda sanjari na kuepuka kuwafanyia vitendo vya ukatili.
Naye Matha Abas ambaye ni mwajiri alikiri kuwa kuajiri watoto wenye umri mdogo kuna changamoto nyingi ikiwamo kutofanya kazi kwa ufasaha, kupenda kucheza na kusahau majukumu yao.
Naye Yohana Ulinda alisema kila mtu anawajibu wa kuajiri wafanyakazi wenye umri mkubwa ili waweze kutambua wajibu wao.
“Inasikitisha kuona kuna baadhi ya watu hupenda kuajiri watoto wadogo kwa sababu ataishi naye kwa muda mrefu na kusahau kufanya hivyo ni kumnyima mtoto huyo haki zake za msingi,”alisema.