21.5 C
Dar es Salaam
Saturday, July 27, 2024

Contact us: [email protected]

Vyuo vikuu vyatakiwa kuzingatia umahiri katika mitaala

Na Mwandishi Wetu, Mtanzania Digital

Serikali imevitaka vyuo vikuu nchini kuzingatia umahiri katika mitaala ili kuendelea kuwa na wataalam wenye uwezo watakaoweza kuleta mabadiliko ya kiuchumi katika Taifa.

Akizungumza katika mahafali ya 19 ya Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA) kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Mwigulu Nchemba, Mhasibu Mkuu wa Serikali, Leonard Mkude, amesema ili kukabiliana na changamoto za usimamizi wa mapato wataalam wanapaswa kuzalisha wahitimu wenye weledi.

“Ili kukabiliana na changamoto za usimamizi wa mapato na matumizi ya fedha za umma, mahitaji ya soko, ushindani na utandawazi tunahitaji wanataaluma wenye weledi, maarifa na umahiri,”amesema Mkude.

Amesema watalaam wanapaswa kuendelea kuzingatia umakini katika mitaala na utoaji wa taaluma ili nchi iwe na wanataaluma ambao wataleta mabadiliko ya kiuchumi kuchochea maendeleo ya nchi.

Mkude pia amewataka wahitimu kujiepusha na vishawishi au vitendo vya rushwa, ubadhilifu na vinginevyo visivyo halali kwakuwa vina madhara makubwa kwao, kwa maisha ya mtu mmoja mmoja na kwa uchumi wa taifa kwa ujumla.

Awali Ofisa Mtendaji Mjuu wa TIA, Dk. Momole Kasambala, amesema taasisi hiyo imeendelea kuboresha mitaala ya elimu ili iweze kuendana na soko la ajira na kuwawezesha wahitimu kujiajri sambamba na kuuhisha mitaala ili kuendana na mabadiliko ya sayansi na teknolojia.

“Kama dira yetu inavyojipambanua kuwa na taasisi inayotoa elimu yenye ubora katika biashara, huduma za utafiti na ushauri barani Afrika, tumejipanga kutoa elimu bora katika jamii,” amesema Dk. Kasambala.

Amesema katika kuinua ubora na ufanisi wa wanachuo wa TIA katika kampasi ya Dar es Salaam imeweza kumalizia maktaba ya kisasa kwenye jengo jipya yenye uwezo wa kuchukua wasomaji 490 kwa wakati mmoja.

Ameongeza pia chuo kimeendelea kuongeza idadi ya vitabu na kompyuta ili kuwawezesha wanachuo kupata huduma bora.

Katika mahafali hayo jumla ya wahitimu 7,131 kutoka Kampasi ya Dar es Salaam na Mtwara walihitimu na kati yao wanawake ni 3,677 sawa na asilimia 51.6 na wanaume ni 3,454 sawa na asilimia 48.4.

Amesema wahitimu hao wametunukiwa cheti cha awali, astashahada, stashahada, shahada na stashahada ya uzamili katika fani mbalimbali.

Waliotunukiwa cheti cha awali ni 2,206, astashahada 1,710, stashahada 1,377, shahada 1,827 na stashahada ya uzamili ni 11.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
589,000SubscribersSubscribe

Latest Articles