28.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

VIONGOZI CHADEMA GEITA WAPATA DHAMANA

Na HARRIETH MANDARI-GEITA

BAADA ya kusota rumande kwa zaidi ya mwezi mmoja, viongozi na wanachama wa Chama cha Demokrasia na Maendelelo (Chadema), waliokuwa wakishikiliwa na polisi kwa kosa la kufanya mkutano bila kibali, wameanza kupata dhamana.

Makada hao wa Chadema wanaodaiwa kukusanyika kwa nia ya kufanya mkutano bila kibali Julai 7, mwaka huu walifikishwa mahakamani juzi mbele ya Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Wilaya ya Chato, Jovit Kato.

Akielezea kupata dhamana kwa makada hao, Katibu wa Chadema Kanda ya Victoria, Rehema  James, alisema washtakiwa hao wamepata dhamana wachache kutokana na kukosekana kwa gari la kutosha kuwabeba wote 40 hivyo kufikishwa mahakamani 14 kutokana na kuchanganywa na wengine 26 wa kesi tofauti waliohitaji kufikishwa mahakamani.

“Tatizo lilikuwa ni kukosekana kwa gari la kuwasafirisha kutoka gereza la Biharamulo kuja mahakamani, sasa polisi mkoani Geita wametoa gari kwa ajili ya kuwachukua mahabusu hao kutoka gerezani lakini kati ya 40 wameletwa 14 mahakamani,” alisema.

Fungu la kwanza la mahabusu wakiwamo viongozi na wanachama 14 lililetwa jana na kuhifadhiwa mahabusu ya kituo cha polisi Chato kusubiri wadhamini wao ambao walitakiwa kufika mahakamani hapo kwa ajili ya taratibu za kudhamini.

Akizungumza na MTANZANIA mara baada ya watuhumiwa hao kutolewa kwa dhamana, Wakili wa watuhumiwa hao, Siwale Yisambi alishukuru Jeshi la Polisi kwa kutoa gari kwa ajili ya utoaji wa dhamana kufanyika.

“Ni kutokana na uhaba wa magari tulielezwa kuwa ili kuwe na utaratibu mzuri wa kuleta mahabusu mahakamani ilibidi kuletwa kwa zamu kwani kulikuwa pia na washtakiwa wengine ambao wanaohitaji kuletwa mahakamani wapate dhamana,”alisema wakili Siwale.

Alisema polisi wamesema gari hilo litaendelea kufanya kazi ya kuwaleta watu mahakamani kwa wiki nzima kwa watuhumiwa wote bila kutoa upendeleo kwa washtakiwa wa Chadema pekee.

“Hadi sasa watuhumiwa ambao bado wapo mahabusu ni 22 ambapo leo (jana) walitoka 15 na hivyo kufanya waliobaki kutojua ni lini watapata dhamana,”aliongeza.

Waliotoka ni wanawake  sita na wanaume saba ambao wote ni wanachama na kiongozi mmoja pekee aliyetoka ni Mange Sayi ambaye ni mwenyekiti wa Chadema Wilaya ya Chato.

Viongozi na wafuasi 51 wa Chadema walikamatwa Julai 7, mwaka huu kwenye ukumbi wa Manzagata kata ya Muganza uliopo wilayani Chato wakiwa kwenye kikao cha ndani na kushtakiwa kwa kosa la kufanya mkusanyiko bila kibali.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles