27.9 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Upelelezi wizi TRA wanoga

IMG_8159Jonas Mushi na Veronica Romwald, Dar es Salaam

JESHI la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam limekamata magari mawili yanayosadikiwa kutumika kubeba vitu vilivyoibwa katika Ofisi ya Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).

Taarifa ya kukamatwa kwa magari hayo imetolewa jana na Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Simon Sirro, katika mkutano na waandishi wa habari uliofanyikia ofisini kwake Dar es Salaam.

Afande Sirro aliyataja magari hayo kuwa ni Toyota Noah lenye namba za usajili T. 989 CNV na Mitsubishi Pajero lenye namba za usajili T. 386 CCV.

“Katika wizi huo vitu vilivyoibwa ni kompyuta mbili aina ya Dell ambazo ziliibwa seti nzima, yaani ‘CPU na Monitor’ na luninga moja aina ya Samsung inchi 40,” alisema Afande Sirro.

Alisema Jeshi la Polisi lilifanikiwa kukamata magari hayo baada ya kupata taarifa za wizi huo kutoka kwa Katibu Muhtasi wa Kamishna Mkuu wa TRA, Matrida Justus, aliyebaini kuvunjwa kwa ofisi yake na wizi kufanyika.

Afande Sirro alisema katika tukio hilo walinzi wawili waliokuwa zamu aliowataja kwa majina ya Joseph Manoti na Hussein Kombo ambao ni walinzi wa Kampuni ya SUMA JKT ndio waliotiwa mbaroni.

Aliwataja watuhumiwa wengine waliokamatwa baadaye wakihusishwa na tukio hilo ni Omary Said (30), Rajabu Said (33) na Vedasto Bernard (56), ambao walikiri kushirikiana wizi huo.

Tukio hilo la wizi lilitokea muda mfupi kabla ya Rais John Magufuli kutangaza kumwondoa kwenye wadhifa Eliakim Maswi, ambaye alikuwa Kaimu Naibu Kamishna wa TRA na kumrejesha katika nafasi yake ya awali ya Katibu Tawala wa Mkoa wa Manyara.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles