23.3 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

UKIJUA LUGHA UNAWEZA KUSOMA KATIKA VYUO HIVI CHINA

Na FARAJA MASINDE


Exif_JPEG_PICTUREKATIKA karne 21 tuliyonayo sasa mwanafunzi ana kila sababu ya kutimiza malengo yake kitaaluma.

Kama ndoto yako ni kubukua nje ya nchi kwenye miji na mataifa yaliyoendelea na bado uko shule basi ondoa shaka.

Kwani kila iitwapo leo mataifa yaliyopiga hatua kubwa kimaendeleo yanakuja na njia mpya za kiubunifu ambazo ni rafiki kwa kila mmoja wetu kuhakikisha kuwa anafikia hatua ya kubukua nje.

Ni wazi kuwa kuna mataifa ambayo yamebahatika kuwa na mazingira mazuri ya kujifunzia hii ikijumuhisha pia kuwa na hali nzuri ya kiuchumi na hata kuwa na njia za kisasa zaidi utoaji elimu.

Wengi wamekuwa wakisaka nafasi ya kwenda kubukua kwenye vyuo vya kimataifa lakini imekuwa si jambo jepesi kama nilivyowahi kueleza kwenye makala zilizopita.

Kuna changamoto kubwa imekuwa ni katika kumudu gharama za masomo, maradhi na hata usafiri ikilinganishwa kuwa fedha ya kitanzania imekuwa haifui dafu pindi unapoibadilisha kwenda fedha za kigeni (Baadhi ya mataifa).

Lakini kuanzia leo tambua kuwa tayari kuna daraja limewekwa kwa ajili yako ili kukuwezesha kwenda kubukua kwenye vyuo bora vya Bara la Asia hususan nchini China.

Daraja hili linatokana na jitihada za dhati ambazo zimewekwa na Taasisi ya Confucius ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ambayo imekuwa ikijishughulisha kufundisha lugha na utamaduni wa kichina kwa miaka kadhaa sasa.

Mkurugenzi wa taasisi hiyo, Profesa Zhang Xaozhen, anasema tayari imeandaa mazingira ya kuhakikisha kuwa wanafunzi kuanzia ngazi ya sekondari hadi vyuo vikuu wanayo fursa ya kwenda kusoma katika vyuo vikubwa vya nchini China huku wakipatiwa ufadhili wa asilimia 100.

Kwa mujibu wa Profesa Zhang, kitu pekee anachotakiwa kufanya mwanafunzi ambaye ndoto yake ni kusoma China ni kuhakikisha kuwa anafaulu kwenye hatua ya mwisho ambayo ni ya sita katika kujifunza utamaduni wa taifa hilo ikiwamo lugha.

“Tunatambua fika kuwa kadri miaka inavyokwenda tunaimani kuwa kufahamu lugha hii ya kichina kutakuwa na faida kwa wanafunzi wa kitanzania walioko kwenye ngazi mbalimbali za elimu.

“Hivyo kupitia Taasisi ya Confucius tumeamua kueneza mafunzo haya ya lugha ya kichina pamoja na tamaduni mbalimbali kuanzia shule za msingi mpaka kwenye baadhi ya vyuo vikuu.

“Kwa wanafunzi wa sekondari na wale wa vyuo kwa wale wanaofaulu vizuri kwenye mtihani wa mwisho ambao ni hatua ya sita wamekuwa wakipata ufadhili wa asilimia 100 wa kwenda kusoma kwenye vyuo mbalimbali nchini China, huku kigezo kikiwa ni kuchukua somo la kichina kwenye fani yoyote atakayochukua,” anasema Profesa Zhang.

Anasema wanafunzi ambao wanaweza kupata mwanya huo ni wale walioko sekondari na vyuo wanaoshindwa kufanya hivyo kwa walioko shule ya msingi kwa sababu bado ni wadogo hivyo hawawezi kumudu kujisimamia wenyewe.

Baadhi ya vyuo ambavyo mwanafunzi anaweza kwenda kusoma nchini China kwa kupitia mgongo huo wa Confucius ni pamoja na Harbin Normal University, Shanghai Normal University, Zhengzhou University, Tianjin University na Beijing Institute University.

Kwasasa taasisi hiyo imeanzisha mpango wa kufundisha utamaduni wa kichina kwenye shule za sekondari ambazo ni Baobab iliyoko Bagamoyo mkoani Pwani, St. Mathew ya Dar es Salaam, King David ya Mtwara huku mkakati ukiwa ni kuzifikia shule nying zaidi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles