23.3 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

TUZO ZA EATV… Kwanini mastaa wametoswa?

dimond

Na JOSEPH SHALUWA

MIONGONI mwa habari zinazobamba kwa sasa katika ulimwengu wa mastaa Bongo ni pamoja na Tuzo za EATV 2016, lakini kinachozunguka zaidi vichwani mwa wadau ni kutoswa kwa baadhi ya mastaa wengi wa filamu na muziki katika kinyang’anyiro hicho.

Tuzo hizo ambazo zinatarajiwa kutolewa Desemba 10, mwaka huu katika Ukumbi wa Mlimani City, jijini Dar es Salaam, washiriki wake walipatikana kwa kujaza fomu wenyewe kabla ya mchujo kupita.

Hata hivyo, baada ya majina ya washiriki wanaoshindana katika vipengele mbalimbali kutolewa, imeonekana kuwa baadhi ya wasanii wakubwa wenye uwezo hawamo kwenye kuwania tuzo hizo.

Kati ya wasanii zaidi ya 1,000 waliojaza fomu za kuomba kushiriki katika tuzo hizo ni wasanii 45 pekee waliotajwa kuingizwa katika shindano ili wapigiwe kura kabla ya washindi kutangazwa kwenye hafla hiyo.

Hizi ni tuzo za kwanza kutolewa na Kampuni ya East Africa TV Limited, ambao ni wamiliki wa vituo vya redio na runinga za East Africa (EA Radio na EATV) huku washiriki wakitakiwa kujaza fomu wenyewe ikiwa wana vigezo vilivyotajwa na waandaaji.

Majina 45 yanayoshindanishwa katika vipengele tisa tofauti yamewashtua wengi, huku baadhi ya wasanii maarufu waliotuma fomu zao wakilalamika kwenye mitandao mbalimbali ya kijamii kuachwa kwenye tuzo hizo ingawa wamekamilisha taratibu zote.

Ili kuondoa utata huo, Swaggaz lilimsaka Seleman Mabiso, ambaye ni mtaalam kutoka Baraza la Sanaa Tanzania (Basata) ili kufafanua kuhusiana na hilo ambapo alisema kuwa, kilichowaponza mastaa wengi ni kutokufuata masharti na vigezo vilivyotolewa kwa washiriki.

“Kwanza, wengi walidharau kushiriki tuzo hizi kwa mtindo wa kujaza fomu, waliamini kuwa na kazi nzuri tu kunatosha kwa waandaaji kuwafikiria na kuwaweka kwenye orodha hata kama hawakuonyesha nia ya dhati ya kushiriki,” alisema Mabiso.

Akaongeza: “Jingine kubwa na la muhimu lilikuwa ni msanii kujisajili kama msanii rasmi kupitia Basata, kigezo ambacho ni muhimu sana katika ushiriki wa tuzo hizi zinazoelekea kuwa na sura ya kimataifa katika miaka ya karibuni.”

Alisema ni kweli wasanii wengi wenye majina walikidhi vigezo vingine kama kuwa na kazi iliyotoka kati ya Julai Mosi, 2015 hadi Juni 30, mwaka huu, yenye umaarufu na inayokubalika na jamii, lakini vigezo vingine muhimu hawakutimiza.

“Lakini hili la kujirasimisha kama mwanasanaa kupitia chombo rasmi cha serikali walilidharau, matokeo yake katika mchujo hawakupita, wakabaki kulalamika lakini ni kitu ambacho walitakiwa kukifanya si kwa sababu ya tuzo, bali kwa faida yao wenyewe na kazi zao,” anasema Mabiso.

Tuzo hizo zilizowashirikisha wasanii mbalimbali kutoka nchi za Afrika ya Mashariki zinatarajiwa kuwa chachu ya mafanikio kwa wasanii wetu wa ukanda huu.

Wasanii na vipengele mbalimbali wanavyoshindana ni kama ifuatavyo:

Joh Makini (Don’t  Bother), Lady Jaydee (Ndi Ndi Ndi), Navy Kenzo (Kamatia chini), Ali Kiba (Aje) na Ben Pol (Moyo Mashine) wanashinda katika kipengele cha Wimbo Bora wa Mwaka.

Tuzo ya Mwanamuziki Bora wa Kiume ni G-Nako, Shettah, Ben Pol, Mwana FA na Ali Kiba wakati Tuzo ya Mwanamuziki Bora wa Kike wakichuana Lilian Mbabazi (Uganda), Ruby, Liana, Vanessa Mdee na Lady Jay Dee.

Kuna Tuzo ya Mwanamuziki Bora Chipukizi, hii inawaniwa na Man Fongo, Feza Kessy ‘Feza’, Rucky Baby, Mayunga na Bright.

Mwigizaji Bora wa Kiume ni Said Ally, Meya Khamis, Daudi Tairo ‘Duma’, Salim Ahmed ‘Gabo’ na Doto Matotola wakati Tuzo ya Mwigizaji Bora wa Kike, Chuchu Hans, Khadija Ally, Kajala Masanja, Rachel Bitulo na Khadija Ally wakipigana vikumbo.

Filamu Bora ya Mwaka ni Hii ni Laana (Kajala Masanja), Nimekosea Wapi (Rachel Kitulo), Safari ya Gwalu (Gabo), Mfadhili Wangu (Daud Michael) na Facebook (Meya Khamis).

Video ya Wimbo Bora ya Mwaka, Ndi Ndi Ndi (Lady Jay Dee), Don’t Bother (Joh Makini), Aje (Ali Kiba), Namjua (Shettah) na Njogereza (Navio – Uganda) huku Kundi Bora la Mwaka wakiwa ni Wakali Wao, Sauti Sol (Kenya), Team Mistari (Kenya), Mashauzi Classic na Navy Kenzo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles