LOS ANGELES, Marekani
STAA wa mchezo wa tenesi anayeshika nafasi ya nne kwenye viwango vya ubora duniani, Stefanos Tsitsipas, atafanyiwa upasuaji wa kiwiko na huenda hiyo ikamtupa nje ya michuano ya Australian Open.
Tsitsipas mwenye umri wa miaka 23, amekuwa akisumbuliwa na maumivu ya kiwiko kwa miezi kadhaa na itakumbukwa alivyojitoa kwenye mashindano makubwa mawili, Paris na Turin.
Sasa, raia wa Ugiriki huyo ni kama ameamua kulifungia kazi tatizo hilo kwa upasuaji anaotarajiwa kufanyiwa na daktari aliyewahi kumtibu mkali mwingine wa tenesi, Novak Djokovic.
Huku Australian Open ikisubiriwa kuanza Januari 17, mwakani, ni ngumu kumuona Tsitsipas akiingia mzigoni kwani anatarajiwa kuuguza jeraha la upasuaji kwa kipindi kisichopungua miezi sita.