23.8 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

TCB yanoa zaidi ya Wanawake 300 Mwanza kushiriki kuinua uchumi wa Taifa

Na Clara Matimo, Mwanza

Katika kuhakikisha wanawake  nchini wanashiriki kujenga na kuinua uchumi wao na  taifa, Benki ya Biashara Tanzania (TCB) imewakutanisha wanawake zaidi ya 300 Mkoani Mwanza na kuwapa elimu ya biashara itakayowasaidia kuzitambua  fursa za kibenki kwa ajili ya maendeleo.

Baadhi ya washiriki wa kongamano la wanawake na biashara  lililofanyika jijini Mwanza leo Oktoba 18, ambalo limeandaliwa na Benki ya Biashara ya Tanzania(TCB) lengo likiwa ni kuwapa elimu  ya biashara itakayowasaidia kuzitambua fursa za kibenki zinazopatikana katika taasissi hiyo ya fedha ili wazitumie  kujikwamua kiuchumi.Picha na Clara Matimo.

TCB imelikutanisha kundi hilo  ikiwa ni mwendelezo wa  kongamano la wanawake na biashara ambalo  ililizundua mwanzoni mwa mwezi huu jijini Dodoma   mada yake kuu ikiwa  ni ‘Nafasi ya Mwanamke katika kukuza Uchumi wa Taifa’ lililolenga kubainisha mahitaji maalumu ya kifedha ya  wanawake na kuwapa fursa kujifunza mambo mbalimbali pia kuijua  benki hiyo na huduma zake.

Akizungumza jijini Mwanza leo  katika kongamano hilo, Kaimu Afisa Mtendaji Mkuu wa TCB, Moses Mnyatta,  amesema pamoja na changamoto nyingi za kifedha walizonazo wanawake watahakikisha ajenda ya kuwawezesha kiuchumi inafikia malengo yaliyokusudiwa kwa kuwaonyesha  fursa  walizonazo na kuwaelimisha jinsi ya kufanya biashara zenye tija.

Mnyatta amesema TCB imejiandaa vizuri kwa hilo kwani  ina fursa lukuki za kibiashara na uwezeshaji kupitia huduma maalumu kama akaunti ya Tabasamu na na suluhishi mbalimbali  kama bima ya nishike mkono na kinamama sera  pia iko imara kifedha , hodari wa kidijitali, bingwa wa ubunifu, wigo mpana wa huduma na mtandao mkubwa wa kuzifikisha popote kwa wakati.

“Tuna mtandao wa matawi makubwa 46, madogo 36, ofisi za wakala za shirika la posta Tanzania 120, ATM 84 ambazo zimeunganishwa na ATM 350 za mtandao wa Umoja Switch hivyo itakuwa rahisi kuwafikia wanawake wengi na kusaidia kuwawezesha kupitia matawi na vituo vyetu vya huduma vilivyosambaa  Tanzania bara na visiwani.

 Mafanikio ya jitihada hizi yatatokana na mpango mkakati tulionao TCB wa kufanya mapinduzi makubwa ya kuwahudumia wanawake, tutatekeleza jukumu hili adhimu kwa kuwa kinara wa huduma jumuishi za kifedha za akina mama na kiongozi mbunifu wa huduma hizo sokoni hili linawezekana kwani mwaka 2007 hadi 2020 mikopo imeongezeka kwa zaidi ya Sh bilioni 580 hadi sasa wanawake ambao ni nusu ya wateja wetu  milioni moja tumeishawakopesha zaidi ya Sh bilioni 120 ,”amebainisha  Mnyatta.

Mgeni rasmi katika kongamano hilo, Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dk. Angeline Mabula,  amesema  serikali itaendelea kusimamia, kupitia  na kutekeleza sheria mbalimbali ambazo zinalenga kumuinua mwanamke kiuchumi.

Amewata TCB kuangalia namna ya kuwafikia wanawake wanaoishi kijijini kwa kupeleka makongamano kama hayo kwenye maeneo ya pembezoni  ili nao wanufaike na  fursa wanazozitoa  kwa kufanya hivyo  hakuna mwanamke atakayebaki  nyuma katika kujiinua kiuchumi yeye na taifa kwa ujumla.

“TCB mmesema kongamano kama hili litaendelea mikoa ya Tanga, Arusha, Dar es Salaam na kule Zanzibar, kama jukwaa la kuwakutanisha wanawake kujifunza mambo mbalimbali na kuijua zaidi benki yenu na huduma mnazozitoa hakika yamekuja muda muafaka yatasaidia serikali kuhakikisha hakuna mwanamke anayeachwa nyuma kiuchumi na kimaendeleo  maana yatabadilisha hadhi ya wanawake nchini kifedha na kiuchumi nawapongeza sana,”amesema.

Nao baadhi ya wanufaika wa mikopo kutoka TCB wameiomba taasisi hiyo ya fedha kuangalia namna ya kupunguza riba pamoja na kuwafikia wanawake wenzao wanaoishi vijijini  ili lengo walilolikusudia la kumuinua mwanamke lifanikiwe kwa asilimi kubwa maana wengi wako maeneo hayo.

  Mkurugenzi wa Shirika lisilo la Serikali linalojishughulisha kuwawezesha wanawake na wasichana kumiliki rasilimali zalishi ili waweze kujikwamua kiuchumi la Mikono Yetu, Maimuna Kanyamala, ameiomba benki hiyo kuwafikia wanawake wa kijijini ambao wanajishughulisha na kilimo ili nao waweze kunufaika na mikopo wanayoitoa kwani yeye ingawa anaishi mjini lakini mkopo aliopata ameutumia katika kilimo na anaendelea kunufaika.

“Wito  wangu kwa TCB ambao wana nia ya kuwasaidia wanawake wawafikie wenzetu wanaoishi kijijini maana wakienda kukopa wanakutana na changamoto nyingi kutoka taasisi za fedha  lakini nao  wana ndoto wana nia pia  wana morali ya kujikwamua kiuchumi wakiwezeshwa mitaji  wanaweza  kuleta mabadiliko chanya katika taifa na familia zao,“amesema Kanyamala.

Khadija Liganga ambaye ni Mkurugenzi Mkuu wa Dida Vitenge wear amesema” Ukiangalia  riba ambayo anaitoa mwanamke mjasiliamali ni sawa na kwamba anachuma kwa ajili ya taasisi  za fedha, tunataka taasisi hizi   ziwe msaada na sio zenyewe zisaidiwe na wajasiliamali.

“Vilevile tukisema tunaenda na mama 2020 basi tuanze na wanawake wa chini ambao pia wanachangia pato la taifa hili ambao wengi wao wanaishi vijijini,’alibainisha Liganga.

Naye Diwani Viti Maalumu (CCM)  kutoka Wilaya ya Ilemela, Winifrida Gyunda, amesema “Changamoto kubwa inayotukabili wanawake ni kuhusu suala zima la kupata mikopo , taasisi nyingi za fedha zimekuwa zikijinasibu kwamba zinatoa mikopo mizuri na kwa haraka lakini tukienda kwenye utekelezaji hii sio halisi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles