25.2 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 23, 2024

Contact us: [email protected]

Tanapa yalipa kodi ya Sh bilioni sita

Pascal SheluteteNA MWANDISHI WETU, ARUSHA

SHIRIKA la Hifadhi za Taifa (Tanapa) limesema kwa mwaka wa fedha wa 2013/2014 lilitumia zaidi ya Sh bilioni sita kama kodi na michango ya maendeleo kwa jamii.

Kauli hiyo ilitolewa mjini hapa jana na Meneja Mawasiliano wa Tanapa, Pascal Shelutete.

Alisema Tanapa inajitegemea kwa asilimia 100 kwa mujibu wa hesabu zake za mwaka 2013/2014 zilizokaguliwa na makusanyo yalikuwa ni Sh bilioni 150.9.

“Makusanyo hayo ya shilingi bilioni 150.9 ni kutoka katika vyanzo mbalimbali vya mapato vya shirika letu la umma ambapo matumizi yalikuwa shilingi bilioni 145.9 huku tukiichangia Serikali Kuu jumla ya shilingi bilioni 6.7 kama kodi,” alisema Shelutete.

Akitoa mchanganuo huo wa kodi hiyo, alisema Tanapa ililipa Sh bilioni 1.5 kama kodi, ikatoa Sh bilioni 2.5 kama michango kwa Mfuko Mkuu wa Hazina pia ikatoa Sh bilioni 1.5 kama mchango wa tozo kwa ajili ya kuendeleza utalii huku Sh bilioni 1.1 zikielekezwa katika miradi ya maendeleo ya jamii inayozunguka hifadhi mbalimbali nchini.

Shelutete alitoa ufafanuzi huo baada ya mapema wiki hii vyombo kadhaa vya habari kuripoti kwamba katika mwaka wa fedha wa 2013/2014, Tanapa ilifanya matumizi makubwa ya fedha zaidi ya mapato yake.

Taarifa hizo ziliwanukuu wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Uwekezaji (PIC) wakisema kwamba katika mwaka huo, taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) ilionyesha kwamba Tanapa ilitumia zaidi ya Sh bilioni 151.7, ilhali mapato yalikuwa ni Sh bilioni 149.9; kukiwa na matumizi ya ziada ya Sh bilioni 1.8.

Pia Shelutete alisema hadi sasa bajeti ya Tanapa si tegemezi.

“Kwa kuzingatia changamoto za uhifadhi, makisio ya gharama za uhifadhi zimeonekana kuwa kubwa kuliko mapato tarajiwa na nakisi iliyojitokeza imelengwa kusaidiwa na wafadhili mbalimbali wa ndani na nje ya Tanzania.

“Shirika huandaa bajeti zake za kila mwaka kwa kuangalia hali halisi ya mapato na matumizi yanayoendana na mapato yake, ikiwa ni pamoja na kukasimia kodi mbalimbali na michango ya Serikali Kuu,” alisema Shelutete.

Alisema Tanapa ina Mpango Mkakati wa Shirika (CSP) wa mwaka 2013/2014 hadi mwaka 2017/2018 ulioandaliwa kwa ajili ya kuonyesha hali halisi na gharama stahiki za uendeshaji wa shughuli za uhifadhi kwa kipindi tarajiwa.

“Tafsiri ya mpango huu katika fedha huchukua taswira ya hali halisi ya changamoto za uhifadhi. Mpango mkakati huo umeandaliwa kwa minajili vile vile ya kuwaeleza wadau wa uhifadhi changamoto na upungufu wa gharama za uhifadhi. Nakisi inaonekana katika mpango mkakati inatarajiwa kufidiwa na wadau wa maendeleo na uhifadhi,” alisema Shelutete.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles