BAADHI ya watu wenye ulemavu, wametoa wito kwa jamii kuenzi na kusapoti maudhui ya Tamasha la Pasaka ambalo limekuwa likifanyika kila mwaka chini ya uratibu wa Kampuni ya Msama Promotions ya jijini Dar es Salaam.
Akizungumza kwa njia ya simu akiwa safarini DR Congo, Esperance Wetewabo ambaye ni mlemavu wa mikono na mguu, alisema jamii ina kila sababu ya kuliunga mkono tukio hilo ambalo mbali ya kuutangaza utukufu wa Mungu, pia sehemu ya mapato imekuwa ikiyafariji makundi maalumu kama walemavu, yatima na wajane.
Alisema mbali ya manufaa mengi ya uwepo wa Tamasha la Pasaka ikiwemo kuchangia kukua kwa muziki wa injili ambao pia umekuwa ajira kwa wenye vipaji, Tamasha hilo pia limekuwa kiunganishi cha ujirani mwema kati ya Tanzania na nchi nyinginezo.