29.2 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

Stewart agundua dosari Azam

Stewart-HallNA MSHAMU NGOJWIKE, DAR ES SALAAM

KOCHA Mkuu wa Azam FC, Stewart Hall raia wa Uingereza, amegundua dosari ndani ya kikosi chake huku akieleza kuwa hajaridhishwa na ubora wa nyota wake kutokana na uwezo walioonyesha katika mechi ya ufunguzi wa michuano ya Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya Tanzania Prisons.

Azam ambao wameanza mkakati wa kuwania ubingwa wa Ligi Kuu Bara baada ya kushindwa kuutetea msimu uliopita, juzi waliwakaribisha Prisons kwenye Uwanja wa Azam, Complex na kufanikiwa kuibuka na ushindi wa mabao 2-1.

Mabao ya Azam katika mchezo huo ambao ulikuwa wa kusisimua yalifungwa na mshambuliaji, Kipre Tchetche raia wa Ivory Coast pamoja na kinda, Farid Mussa, huku la kufutia machozi kwa Prisons likiwekwa wavuni na Jeremia Juma.

Akizungumza na MTANZANIA mara baada ya mchezo huo, Stewart alisema wachezaji wake walipoteza nafasi nyingi za kufunga na hata safu ya ulinzi haikufanya vizuri jambo lililomfanya asifurahie kabisa mechi hiyo ya ufunguzi wa ligi.

“Siwezi kusema kikosi changu kipo vizuri kwani kuna makosa mengi yamejitokeza leo (juzi) ambayo kama tungekuwa tunacheza na timu imara yangetugharimu sana,” alisema.

“Kwa jinsi Prisons walivyotusumbua inabidi kuyafanyia kazi haraka makosa yaliyojitokeza kabla ya kucheza na Stand United mechi inayofuata ambayo tutakuwa ugenini kwenye Uwanja wa Kambarage, Shinyanga,” alisema.

Stewart ambaye amerejea Azam baada ya Mcameroon, Joseph Omog, kutimuliwa alisema changamoto waliyoipata kwa Prisons inaonyesha ni jinsi gani ligi itakavyokuwa ngumu msimu huu kwani kila timu imejiandaa kupambana kupata ushindi.

Mabingwa hao wa Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati (Kombe la Kagame), watashuka tena dimbani keshokutwa kuvaana na Stand United ambao walianza ligi hiyo kwa kupata kipigo cha bao 1-0 dhidi ya Mtibwa Sugar nyumbani.

Azam wanatarajiwa kuondoka leo kuelekea mkoani Shinyanga kujiandaa na pambano lao dhidi ya wenyeji, Stand United.

 

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles