27.5 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Siri JPM kutumbua Bodi  TRA hii hapa

0d6a8531VERONICA ROMWALD Na JONAS MUSHI

  • DAR ES SALAAM

SIRI ya kutenguliwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Bernard Mchomvu na bodi nzima ya wakurugenzi imeelezwa  kuwa ni kutokana na kushindwa kutimiza malengo ya Serikali ya kukusanya mapato ya kutosha.

Chanzo kimoja cha habari kutoka ndani ya TRA kiliiambia MTANZANIA kuwa huenda Bodi hiyo imeshindwa kubuni mikakati madhubuti ya kukusa mapato tofauti na matarajio ya Serikali ya Dk. John Magufuli ya kuhakikisha nchi inajitegemea kupitia vyanzo na mapato yake ya ndani.

Pia hatua hiyo ya Rais kutengua Bodi hiyo imechukuliwa siku chache tangu itolewe ripoti ya hali ya uchumi ya Septemba mwaka huu ambayo ni robo ya kwanza ya mwaka wa bajeti wa 2016/2017.

 

Taarifa nyingine zinadai huenda Bodi hiyo imetumbuliwa baada ya kutoa mapendekezo mbalimbali juu ya utozaji wa kodi kwenye mizigo nje ya nchi (on transit) pamoja na tozo za mipakani jambo ambalo uongozi wa juu wa serikali umeona ushauri huo hautekelezeki.

Mapendekezo ya Bodi hiyo yalieleza kuwa kodi hizo zimekuwa zikichangia kushuka kwa uchumi wa nchi.

Taarifa ya Rais iliyotumwa kwenye vyombo vya habari na kusainiwa na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais Gerson Msigwa, Ikulu jana, ilisema uteuzi wa mwenyekiti mpya   na bodi hiyo utatangazwa baadaye.

Hata hivyo taarifa hiyo ya Ikulu haikutaja sababu za kutenguliwa  Bodi hiyo ya TRA.

Taarifa hizo zinadai kuwa kuhusu tozo inayojulikana kama “on transit VAT”, bodi hiyo ilipendekeza iondolewe na badala yake uwekwe utaratibu mzuri wa kuyabaini magari ambayo kweli yanatoka Bandari ya Dar es Salaam kwenda nchi za Maziwa Makuu  kuepuka udanganyifu unaoweza kujitokeza.

Ilidaiwa kwamba Bodi hiyo ilipendekeza pia uwekwe utaratibu mzuri utakaowezesha mfumo wa kukusanya mapato ya mipakani  ufanyike haraka  kuepuka ucheleweshaji usio na msingi kwa wafanyabiashara wa nje.

Chanzo hicho kilidai kuwa licha ya mchanganuo na ushauri huo, Serikali haikukubaliana na ushauri huo Bodi.

“Inawezekana ushauri huo haukukubaliwa na ilionyesha uongozi wote wa Bodi umeshindwa kazi na hauwezi kwenda na kasi ya serikali ya sasa.

Ingawa Rais Magufuli alitoa mwezi mmoja kwa wafanyabiashara wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) kutumia Bandari ya Dar es Salaam bila tozo mbalimbali, bado wafanyabiashara hao hawakuchangamkia ofa hiyo na wameendelea kutumia bandari nyingine zikiwamo   Beira,   Msumbiji na Mombasa, Kenya.

Taarifa nyingine zinaeleza kuwa huenda pia Ikulu imechukua uamuzi huo kwa kutoridhishwa na   mwenendo wa ukusanyaji wa mapato ambayo yanaonekana kushuka.

Mkurugenzi wa Huduma kwa Malipa Kodi wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Richard Kayombo, hakupatikana  kuzungumzia suala hilo kwa vile  simu yake iliita bila kupokewa.

IKULU YAKANA

Alipoulizwa kuhusu sababu za Rais kutengua uteuzi wa mwenyekiti na kuvunja Bodi nzima ya TRA, Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu, Gerson Msigwa alisema hajui sababu za uamuzi huo.

“Mimi ninachojua ni kwamba Rais ametengua uteuzi wa Mwenyekiti wa Bodi ya TRA na wajumbe wake, lakini hizo sababu nyingine unazoniambia kawaulize hao waliokupa taarifa hizo.

“Unajua siku hizi mtu anaweza kuamua kuandika kwenye mtandao kwamba Msigwa kafa wakati si kweli, mimi sina taarifa nyingine zaidi ya hiyo,” alisema Msigwa.

 

Ripoti ya BoT

Ripoti ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT), iliyotolewa Oktoba  mwaka huu inaonyesha kwamba makusanyo ya mapato ya ndani ya Septemba yalishuka kwa asilimia 16.

Inaeleza kuwa Sh trilioni 1.4 au asilimia 84 ya lengo katika kipindi hicho, zilikusanywa.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo, mapato yaliyokusanywa na Serikali Kuu yalikuwa ni Sh trilioni 1.3 ambazo  ni asilimia 84.3 ya lengo.

Ilieleza kuwa mapato yaliyotarajiwa kukusanywa na serikali za mitaa kwa mwezi huo yalikuwa ni Sh bilioni 55.5 hata hivyo zilizokusanywa ni Sh bilioni 41.2 pekee.

Ripoti hiyo inaonyesha   mapato yasiyokuwa ya kodi yaliyokusanywa katika kipindi hicho ni Sh bilioni 82.2 tofauti na lengo la Sh bilioni 225.7.

Vilevile, makusanyo ya kodi ya mapato yalishuka kwa asilimia 10 ya lengo la Sh bilioni 573.6.

Fedha za miradi kutoka nje zilizopatikana kwa kipindi hicho ni Sh bilioni 100.6 tofauti na lengo la Sh bilioni 993.6.

Ripoti ya BoT ya hivi karibuni inaonyesha kiwango cha makusanyo ya mapato ya serikali katika kipindi hicho yameshuka na hivyo kusababisha ukosefu wa fedha za kutekeleza miradi ya maendeleo.

Taarifa ya kushuka huko kwa makusanyo ya kodi, inaonyesha wazi kuwa imeishtua mamlaka za juu na sasa imeanza kuifanyia kazi.

Katika hatua hiyo, TRA imeanzisha oparesheni maalumu ya ukusanyaji kodi ambayo inakwenda hadi usiku.

Maofisa wake huenda katika maeneo mbalimbali hususan kwenye majengo marefu, maeneo ya sinema na starehe nyingine kwa ajili ya kufanya ukaguzi.

Gazeti dada la MTANZANIA, Mtanzania Jumapili, juzi liliwashuhudia baadhi ya maofisa wa TRA wakiwa katika jengo la Dar Free Market kufanya ukaguzi huku kukiwa na ulinzi mkali wa polisi.

Wakati huo huo, Dk. Magufuli jana alimteua Charles Kichere kuwa Naibu Kamishna Mkuu wa TRA kujaza nafasi hiyo iliyokuwa wazi kwa zaidi ya mwaka mmoja. Taarifa ya Ikulu iliyosainiwa na Msigwa ilisema uteuzi huo unaanza mara moja.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles