Na Ibrahim Yassin, RUNGWE
SERIKALI Wilaya ya Rungwe mkoani Mbeya, imepiga marufuku watu kutoa msaada wa shuka na blanketi katika misiba ili kuepusha ugomvi kwa wanandugu baada ya msiba kumalizika.
Hatua hiyo ya Serikali imekuja baada ya kutokea ugomvi wa mara kwa mara kwa ndugu kugombea vitu hivyo vinavyopelekwa misibani wanapofiwa na kuleta uhasama katika koo mbalimbali.
Aidha, badala ya kuendeleza mila hiyo ambayo inadaiwa imepitwa na wakati wametakiwa kupeleka vyakula ili viwasaidie wakati wa msiba.
Mwenyekiti wa Kitongoji cha Ibungu, Daniel Mwakalinga, alisema kuna baadhi ya familia zimekuwa na uhaba wa chakula na kulazimika kuuagiza uongozi wa Serikali za vitongoji kutoa fedha, huku wananchi wakipeleka nguo, mablanketi na mashuka kuwahani wafiwa.
“Wananchi wanatakiwa watii agizo hilo ili kuepusha migogoro inayoepukika, kinyume na hivyo sheria itachukua mkondo wake ikiwamo kutozwa faini kwa yeyote atakayebainika kuendeleza mila hizo,” alisema.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kijiji cha Ikubo, Edward Mwaisango, alisema kuendekezwa mila za kupeleka vitu hivyo misibani hakuna tija badala yake walengwa hao wasaidiwe wanapokuwa hai.
“Wananchi wanapaswa kupeleka vyakula kama sukari, mahindi, mchele na fedha ambapo kwa kufanya hivyo kunaweza kusaidia wafiwa wakati wa msiba,” alisema.
Kutokana na agizo hilo, baadhi ya wananchi wamejikuta katika wakati mgumu wa kushindwa kutekeleza mila hiyo na wametaka jamii ielimishwe misaada ya kuchangia kabla ya misiba kutokea.
“Ni jambo zuri Serikali kukataza vitendo hivyo, lakini pia jamii ielimishwe kutoa misaada ya matibabu kwa wagonjwa kabla hawajafariki badala ya kupeleka vitu hivyo pindi mgonjwa anapofariki,” alisema mmoja wa wakazi hao, Elias Asajile.