NA ESTHER MNYIKA, DAR ES SALAAM
SERIKALI imezifungia redio 28 kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo kushindwa kulipa ada za leseni na kutimiza masharti yaliyowekwa na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA).
Akizungumza jana jijini Dar es Salaam, Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Professa Makame Mbarawa, alisema majina ya redio zilizofungwa yatatangazwa baadaye na TCRA.
“Natoa agizo kwa kampuni mbalimbali kulipa ada za leseni kwa wakati ambao umepangwa na TCRA na ambao hawatatekeleza agizo hilo watachukuliwa hatua za kisheria,” alisema Profesa Mbarawa.
Wakati huo huo, Serikali imeifungia Kampuni ya Six Telecom Tanzania Limited kutokana na kudaiwa Sh bilioni 7.2.
Waziri Mbarawa alisema kampuni hiyo imebainika kufanya makosa mbalimbali ikiwemo kushindwa kulipa ada za leseni zenye thamani ya Sh bilioni moja.
Profesa Mbarawa alisema kwa sababu hizo Serikali imeifunga kampuni hiyo na tayari imewafikisha polisi baadhi ya watumishi wake kwa ajili ya kuchukuliwa hatua za kisheria.