27.1 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Samatta, Ulimwengu waikosa Barcelona

Samatta-UlimwenguBADI MCHOMOLO, DAR ES SALAAM

NDOTO za Watanzania Mbwana Samatta na Thomas Ulimwengu wanaokipiga TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo kucheza na Barcelona zilizimwa jana na Sanfrecce Hiroshima ya Japan.

TP Mazembe ambao ni mabingwa wa Afrika ngazi ya klabu ilipokea kipigo cha mabao 3-0 dhidi ya wapinzani wao katika michuano ya Klabu Bingwa Dunia inayoendelea nchini Japan.

Mazembe waliweza kumiliki mchezo huo kwa dakika 40 za kipindi cha kwanza kabla ya kuruhusu wapinzani wao kupata bao la kwanza dakika ya 44 ambalo liliwekwa wavuni na mshambuliaji Tsukasa Shiotani.

Kipindi cha pili kilianza kwa Mazembe kuonyesha udhaifu katika safu ya ulinzi hali iliyowapa wapinzani nafasi ya kuongeza bao la pili dakika ya 56, lililofungwa na Kazuhiko Chiba, kabla ya Takuma Asano kufunga bao la tatu.

Katika mchezo huo, Samatta alipata nafasi ya kuanza lakini hakuwa na madhara mbele ya walinzi wa Sanfrecce Hiroshima, ambao waliweza kupambana na kumkaba wakijua uwezo wake lakini Ulimwengu alipata namba kipindi cha pili alipoingia kuchukua nafasi ya Given Singuluma dakika ya 46.

Hata hivyo, Ulimwengu alionyesha cheche zake kwa kujaribu kupiga shuti kali, lakini halikuwa na madhara kwa wapinzani wao.

TP Mazembe ilifanikiwa kushiriki michuano hiyo baada ya kutwaa Kombe la Ligi ya Mabingwa Afrika kwa kuifunga klabu ya Algers ya nchini Nigeria kwa jumla ya mabao 4-1.

Kutokana na matokeo ya jana, TP Mazembe imepoteza ndoto zake za kukutana na mabingwa wa Ulaya, Barcelona iliyosheheni wachezaji nyota kama vile Lionel Messi, Luis Suarez na Neymar.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles