23 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Sakata la Messi latinga TFF

MESSI GOALABDUCADO EMMANUEL NA MWALI IBRAHIM, DAR ES SALAAM
SAKATA la winga wa timu ya Simba, Ramadhan Singano ‘Messi’, akidai mkataba wake umechezewa na klabu yake hiyo sasa limefika rasmi kwenye Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) ili utata wake kumalizwa.
Messi amekuwa na mvutano mkubwa na klabu yake akidai mkataba wake wa miaka miwili umechezewa kwa kuongezewa mwaka mmoja zaidi unaoisha Julai mwakani, tofauti na ule alionao yeye unaomalizika mwezi ujao.
Katibu Msaidizi wa Chama cha Wanasoka Tanzania (Sputanza), Abeid Kasabalala, aliliambia MTANZANIA kuwa wameshayafanyia kazi malalamiko hayo ya Messi kwa mujibu wa vielelezo alivyoviwasilisha na jana asubuhi wamelipeleka suala hilo TFF kwa ajili ya kufanyiwa uamuzi.
“TFF ndio wenye mpira wao, tumelipeleka suala hilo huko leo asubuhi (jana), wenyewe wamelichukulia kwa uzito mkubwa na wameahidi kulifanyia kazi kwa haraka kwa kulipeleka kwenye kamati husika.
“Suala hilo limefika sehemu nzuri kwani kilichopo TFF watalinganisha mikataba waliyokuwa nayo na ile ya Messi ambayo inadaiwa kuwa na utata, wala hamna kazi kubwa sana tunaamini haki itatendeka,” alisema.
Uongozi wa Simba kupitia Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano, Haji Manara, jana ulisema kuwa haujachezea mkataba wa nyota huyo huku ukifika mbali zaidi na kudai wapo kwenye mchakato wa kumwadhibu Messi kutokana na kuichafua klabu hiyo.
Manara pia alieleza kuwa wanaiomba TFF kutoa tamko kuhusu sakata hilo, kwani wana vielelezo vyote vya mikataba wanayoingia na wachezaji wao akiwemo Messi, huku wakidai wapo tayari suala hilo lichunguzwe na vyombo vya dola.
Azam FC imeonyesha nia ya kumsajili Messi lakini wamedai kuwa hawataanza taratibu zozote za usajili wake mpaka pale matatizo na klabu yake yatakapomalizika.
Simba kushusha kifaa Juni 16
Wakati huo huo mshambuiaji mahiri wa timu ya Taifa ya Burundi na klabu ya Vital, ‘O Laudit Mavugo, anatarajia kutua rasmi Simba Juni 16 mwaka huu kumalizana na timu hiyo tayari kwa kujiunga na wenzake kwenye maandalizi ya michuano ya Kagame inayotarajia kuanza Julai 12, Dar es Salaam.
Akizungumza na MTANZANIA jana, Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya klabu hiyo, Zacharia Hanspoppe, alisema asilimia kubwa ya mazungumzo yao na mchezaji huyo yamekamilika kinachosubiriwa ni yeye kutua nchini na kutia saini mkataba wake.
“Tumeamua kumwacha kwa muda ili kuweza kukamilisha ratiba ya michuano na timu yake ya Taifa, baada ya hapo atatua nchini kwa ajili ya kukamilisha taratibu zilizobakia,” alisema.
Alisema kwa sasa wamejipanga kufanya usajili kwa utulivu na hawataki kukurupuka, kwani wanahitaji mabadiliko kuanzia kwenye michuano hiyo ya kiamataifa hadi ya Ligi Kuu Tanzania Bara msimu wa 2015/2016.
Hadi sasa Simba imesajili wachezaji Mohamed Fakhi (JKT Ruvu), Samir Nuhu (Azam), Mohamed Abraham (JKU Zanzibar), Peter Mwalyanzi (Mbeya City) na Mussa Hassan ‘Mgosi’ (Mtibwa).
Wakati wakijiandaa na michuano hiyo, hatima ya kupatikana kwa kocha mpya, wachezaji watakaoiaga timu hiyo na watakaoenda kwa mkopo kwenye timu nyingine itapatiwa ufumbuzi kwenye kikao cha ndani cha klabu hiyo, kilichofikia tamati jana baada ya kudumu kwa muda mrefu.
Timu hiyo inatarajia kuanza mazoezi rasmi Jumatatu wiki ijayo Uwanja wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), kujiandaa na michuano hiyo ya Kagame.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles