27.5 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

RUWASA wajipanga kumaliza kero ya maji Tabora

Na Allan Vicent, Tabora

WAKALA wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) mkoani Tabora wanatarajia kutumia kiasi cha sh bil 32.1 kutekeleza miradi mipya 41 ya maji vijijini na shughuli nyingine za wakala huo katika mwaka huu wa fedha.

Hayo yamebainishwa juzi na Meneja wa RUWASA Mkoani hapa Mhandisi Hatari Kapufi alipokuwa akitoa taarifa katika kikao cha wadau wa maji kilichofanyika katika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa.

Alisema kuwa serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan imekusudia kumaliza kero ya maji kwa wakazi wa vijijini kwa kutekeleza miradi mbalimbali ya kimkakati ikiwemo uchimbaji visima virefu.

Alibainisha kuwa kwa mwaka jana pekee jumla ya miradi 47 ilitekelezwa katika vijiji mbalimbali vya mkoa huo ambapo baadhi imekamilika na mingine iko katika hatua za mwisho, takribani Sh bil 3.3 zimetumika sawa na asilimia 26 ya fedha zote zilizotolewa na serikali.

Kapufi aliongeza kuwa kwa mwaka huu wa fedha jumla ya miradi 29 imetangazwa na kati ya hiyo 7 imetangazwa na Makao Makuu na inakisiwa kugharamu kiasi cha sh bil 12.1 na miradi 22 yenye thamani ya Sh bil 7.3 imetangazwa ngazi ya Mkoa.

Alibainisha kuwa zabuni zingine 12 zinazokisiwa kugharimu Sh bil 10.1 zinatarajiwa kutangazwa hivi karibuni ambapo 10 zitatangawa na Mkoa na 2 zitatangazwa na RUWASA Makao Makuu.

‘Tayari mikataba 10 yenye jumla ya miradi 18 itakayogharimu kiasi cha sh bil 5.2 imesainiwa kwa ajili ya kuanza utekelezaji katika vijiji 44 ambapo zaidi ya wakazi 123,753 watanufaika na miradi hiyo’, alisema.

Mhandisi Kapufi alifafanua kuwa mikataba 2 ya uletaji mabomba na pampu kupitia miradi ya Uviko 19 yenye thamani ya sh bil 1.9 imeshasainiwa na Makao Makuu hivyo kufanya miradi ya UVIKO 19 kughrimu sh bil 4.9.

Alieleza kuwa mikataba 5 kati ya hiyo itatekelezwa kwa fedha za Mpango wa Maendeleo kwa Ustawi wa Taifa (UVIKO 19) kwenye majimbo 10 ya uchaguzi   vijijini na 5 itatekelezwa kupitia Program ya Malipo kwa Matokeo (PforR).

Alisisitiza kuwa ukamilifu wa miradi hiyo utaongeza kwa kiasi kikubwa upatikanaji huduma ya maji safi hadi kufikia asilimia 68.7, aidha vijiji visivyokuwa na huduma ya maji kabisa vitapungua kutoka 200 hadi 156.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles