23.5 C
Dar es Salaam
Thursday, July 4, 2024

Contact us: [email protected]

Rais Samia Mgeni Rasmi Maadhimisho ya Miaka 69 ya Jumuiya ya Wazazi

Na Ramadhan Hassan, Dodoma

Rais wa Tanzania, Dk. Samia Suluhu Hassan, anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika maadhimisho ya miaka 69 ya Jumuiya ya Wazazi, tangu kuanzishwa kwake mwaka 1977.

Akizungumza na waandishi wa habari leo, Jumatatu, Juni 24, 2024, jijini Dodoma, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi Taifa, Fadhil Maganya, amesema maadhimisho ya wiki ya wazazi kitaifa yatafanyika katika Mkoa wa Katavi, Wilaya ya Mpanda, kuanzia Julai 13 hadi 15, mwaka huu.

Maganya, ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM, amesema kwa mwaka 2024, Jumuiya inaadhimisha miaka 69 ambapo baada ya maadhimisho hayo, sherehe zitafanyika katika ngazi mbalimbali za uongozi nchini kote, kuanzia ngazi ya tawi, kata, wilaya, na mkoa.

Maganya amesema wanatarajia kufanya ufunguzi wa maadhimisho hayo Julai 8, mwaka huu, katika Mkoa wa Katavi, Wilaya ya Mlele, Kata ya Inyonga kwenye viwanja vya Shule ya Msingi Inyonga.

“Katika wiki hiyo, tutaitumia kwa kupanda miti zaidi ya 100,000, lengo likiwa ni kutunza mazingira,” amesema Maganya.

Amesema Julai 10, kutakuwa na Baraza Kuu la kawaida la Umoja wa Wazazi Tanzania, Julai 11, kongamano la maadili na malezi, na Julai 12 itakuwa maalum kwa ajili ya michezo.

Mwenyekiti huyo ameeleza kuwa kauli mbiu ya sherehe hizo kwa mwaka 2024 ni “Uchaguzi 2024/2025, Jumuiya ya Wazazi iko mstari wa mbele.”

Katika hatua nyingine, Maganya amempongeza Mkuu wa Wilaya ya Ubungo, jijini Dar es Salaam, Hassan Bomboko, na Mkuu wa Mkoa, Albet Chalamila, kwa kusimamia maadili kwa kukamata madada poa.

Amesema Jumuiya ya Wazazi ina dhamana ya kusimamia maadili, elimu, malezi, mazingira na afya, hivyo kumekuwa na malalamiko kwa Mkuu wa Wilaya hiyo, Bomboko, kwa kushughulikia kinadada wanaouza miili wakitaka kulipwa fidia.

“Kwa niaba ya Jumuiya, tunatoa kauli ya kumuunga mkono na kumpongeza Mkuu wa Wilaya ya Ubungo kwa kazi nzuri anayoifanya na tunatoa wito kwa viongozi wengine kuendelea kufanya kazi kwa kusimamia sheria,” amesema Maganya na kuongeza:

“Haiwezekani mambo ya hovyo yanafanyika na sisi tunayaona na kuyasikia lakini tumekaa kimya. Hivyo, Jumuiya ya Wazazi tutakuwa pamoja na serikali kwa hatua yoyote itakayochukuliwa kuhusiana na suala hili la biashara ya dada poa,” amesema Mwenyekiti huyo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
589,000SubscribersSubscribe

Latest Articles