Na Shomari Binda, Musoma
Mbunge wa Musoma Vijijini, Prof. Sospeter Muhongo, amewaomba wadau wa elimu na wananchi wa Kata ya Nyakatende kuungana kukamilisha ujenzi wa shule ya sekondari Kigera.
Hadi sasa mbunge huyo amechangia mifuko 150 ya saruji kwenye ujenzi wa shule hiyo ikiwa ni kuhakikisha ifikapo mwakani wanafunzi wa kidato cha kwanza wapatao 191 wanaanza masomo.
Kata ya Nyakatende yenye vijiji 4 ina shule moja ya Sekondari hali inayopelekea wanafunzi kutembea zaidi ya kilometa 10 kwenda shule hali iliyopelekea mbunge huyo kuwaomba wadau na wananchi kuchangia kukamilisha ujenzi wa sekondari hiyo.
Prof. Muhongo amesema elimu ni Jambo la muhimu na kazi inayofanyika kwa sasa katika jimbo la Musoma Vijijini ni ukamilishwaji wa majengo ya madarasa ili wanatunzi wote waliofaulu waende shuleni mwakani.