27.5 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Pluijm atoa mbinu za ushindi Rwanda

Hans-Van-De-PluijmNA JENNIFER ULLEMBO, DAR ES SALAAM

KOCHA Mkuu wa Yanga, Hans Van der Pluijm, ameeleza kuwa kwa kufahamu ugumu wa mchezo wao wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya APR Jumamosi hii Uwanja wa Amahoro, Rwanda, anadhani njia pekee ya kuwaliza Wanyarwanda hao ni kufunga mabao ya mbali ili kuweza kuondoka na ushindi ugenini.

Yanga inatarajiwa kuondoka nchini leo asubuhi kuelekea Rwanda ikiwa na wachezaji 20 na viongozi 10 kwa ajili ya mchezo huo wa raundi ya kwanza, baada ya kuitoa Cercle de Joachim ya Mauritius kwenye hatua ya awali kwa ushindi wa jumla wa mabao 3-0.

Wachezaji watakaoondoka ni Ally Mustafa ‘Barthez’, Deogratius Munishi, Oscar Joshua, Deus Kaseke, Kelvin Yondani, Mbuyu Twite, Haruna Niyonzima, Vicent Bossou na Donald Ngoma.

Wengine ni Juma Abdul, Thabani Kamusoko, Pato Ngonyani, Malimi Busungu, Amisi Tambwe, Mwinyi Haji, Said Juma, Paul Nonga, Simon Msuva, Geofrey Mwashiuya na Matheo Anthony.

Akizungumza na MTANZANIA jana, Pluijm alisema kutokana na kucheza ugenini, vijana wake wanatakiwa kutumia ipasavyo nafasi yoyote wanayoweza kuipata ili kuvuna mabao ambayo yatakuwa mtaji wao tosha kuelekea mchezo wa marudiano utakaopigwa jijini Dar es Salaam wiki mbili zijazo.

“Nadhani tukitumia njia hii ya kufunga mabao ya mbali tutaibuka na ushindi, siyo lazima kusubiri hadi ukaribie goli ndiyo utoe pasi au kufunga.

“Kupitia kikao kilichofanyika juzi nilizungumza na wachezaji wangu na kuwapa maelekezo ya kufunga mabao ya mbali, naona wameanza kuyafanyia kazi na imesaidia sisi kuibuka na ushindi wa mabao 5-0 dhidi ya African Sports,” alisema Pluijm.

Pluijm alisema anawaamini wachezaji wake na anatambua kiwango chao ni kizuri, hivyo watampa matokeo mazuri katika mchezo huo.

Wakati huo huo wawakilishi wengine wa Tanzania katika michuano ya kimataifa, Azam FC waliondoka nchini jana kuelekea Johannesburg, Afrika Kusini kwa ajili ya kuikabilia Bidvest Wits katika michuano ya Kombe la Shirikisho.

Timu hiyo imeondoka ikiwa na jumla ya wachezaji 24 tayari kwa mchezo huo unaotarajiwa kufanyika Jumamosi jioni katika Uwanja wa Bidvest.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles