23.4 C
Dar es Salaam
Saturday, April 27, 2024

Contact us: [email protected]

OMOG AIPIGA MKWARA YANGA

img_7362

Na THERESIA GASPER-DAR ES SALAAM

KOCHA Mkuu wa timu ya Simba, Joseph Omog, amewapiga mkwara watani wao wa jadi, Yanga na kuwataka wasahau kuongoza katika msimamo wa Ligi Kuu Tanzania Bara, kwani hawezi kukubali kuwapa nafasi hiyo.

Simba wanashikilia usukani wa ligi hiyo baada ya kujikusanyia pointi 35 katika mzunguko wa kwanza, wakifuatiwa na mabingwa watetezi, Yanga, waliofikisha pointi 33.

Matokeo ya Simba kufungwa michezo miwili mfululizo dhidi ya African Lyon na Tanzania Prisons, yaliwafurahisha mahasimu wao, jambo ambalo limemfanya Omog awashtukie na kuanza kuwapigia hesabu ili wasipate nafasi ya kuongoza ligi.

Akizungumza na MTANZANIA jana, Omog alisema wapinzani wao walimaliza kwa kasi duru ya kwanza, hali iliyomfanya azidishe programu za mazoezi kwenye kikosi chake ili kuwaweka wachezaji fiti zaidi.

Kocha huyo raia wa Cameroon anayesaidiwa na Mganda Jackson Mayanja, alisema wataongeza juhudi ili waweze kufanya vizuri katika michezo yote ya mzunguko wa pili.

“Hatupo tayari kushuka kileleni mwa msimamo wa ligi, licha ya kutofautiana kwa pointi mbili na mahasimu wetu, tukiruhusu makosa hayo yafanyike tutapata presha zaidi,” alisema.

Omog alikiri kuwa mzunguko wa pili wa ligi utakuwa na changamoto nyingi, kutokana na kikosi chake kumaliza vibaya duru la kwanza, huku akiwataka wachezaji kujituma uwanjani na kufanyia kazi majukumu wanayopewa.

Alisema kupitia michezo ya kirafiki waliyocheza, ametambua mapungufu mengi yaliyopo na tayari ameanza kuyafanyia kazi, kabla ya kuanza kwa mzunguko wa pili wa ligi Jumamosi hii.

Wekundu hao wa Msimbazi wanatarajia kuanza duru la pili kwa kumenyana na Ndanda FC ugenini katika Uwanja wa Nangwanda Sijaona, Mtwara.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles