33.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Olivier Giroud aibeba Arsenal Old Trafford

arsenals-olivier-giroud-celebrates-after-the-gameMANCHESTER, ENGLAND

MICHUANO ya Ligi Kuu nchini England iliendelea jana kwenye viwanja mbalimbali, huku mchezo ambao uliteka hisia za watu wengi ni kati ya Manchester United ambayo ilikuwa kwenye uwanja wa nyumbani wa Old Trafford dhidi ya wapinzani wao, Arsenal, ambapo mchezo huo ulimalizika kwa sare ya 1-1.

Ni wazi kwamba, Manchester United walichezea shilingi chooni kutokana na kulazimishwa sare hiyo. United walikuwa wa kwanza kupata bao, ambalo liliwekwa wavuni na kiungo mshambiliaji, Juan Mata, katika dakika ya 68 kutokana na kazi safi ambayo ilifanywa na Paul Pogba, akisaidiana na Ander Herrera, kisha Mata kuumalizia wavuni.

Katika mchezo huo, mashabiki wengi waliwapa Arsenal nafasi ya kushinda kutokana na ubora wao, ambao wameuonesha katika michezo ya hivi karibuni, lakini katika mchezo huo wa jana Manchester United walionekana kuutawala kwa kiasi kikubwa, japokuwa walilazimishwa sare.

Safu ya ushambuliaji ya Arsenal ilionekana si tishio kwa kipindi cha kwanza, kwa kuwa mshambuliaji wao, Alexis Sanchez, alionekana kucheza peke yake, hivyo walinzi wa United walikuwa imara kupambana na mshambuliaji huyo kwa dakika 45 za mwanzo.

Kipindi cha pili kocha wa Arsenal, Arsene Wenger, alifanya mabadiliko katika safu ya ushambuliaji, ambapo alimpa nafasi nyota wake, Olivier Giroud, kwa ajili ya kumuongezea nguvu Sanchez, hivyo Giroud aliweza kuzinyamazisha kelele za mashabiki wa Man United katika dakika ya 89, ambapo aliutumia vizuri mpira ambao ulipigwa na Alex Oxlade-Chamberlain, baada ya kumtoka Marcus Rashford, hivyo mpira huo ulikwenda moja kwa moja na kukutana na Giroud, ambaye alipachika bao kwa kichwa.

Sifa za pekee ziende kwa Giroud, ambaye alionesha jitihada za dhati kuhakikisha anapiga kichwa mpira huo ambao ulipigwa juu, lakini mchezaji huyo aliruka zaidi na kufanikiwa kuugonga kichwa.

United walishindwa kutumia dakika za lala salama kuweza kutamba kwenye uwanja wa nyumbani, kwa kuwa inaonesha wazi Rashford alipitwa kwa urahisi dhidi ya Chamberlain, ambaye alipiga mpira wenye madhara.

Hata hivyo, Rashford alicheza katika kiwango cha hali ya juu katika kusaidia mashambulizi, huku akisaidiana na Mata, lakini walishindwa kuzitumia nafasi ambazo walizitengeneza.

Kiungo ambaye alisajiliwa kwa fedha nyingi katika klabu ya Man United, Pogba, hakuonesha uwezo wake kama watu wengi walivyodhania, mara nyingi alionekana kupoozesha mipira, hivyo mashambulizi yakawa yanafanywa na Mata na Rashford.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles