25.7 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Mwili wa Sitta kuwasili nchini kesho

 Samuel Sitta
Samuel Sitta

LEONARD MANG’OHA, DAR ES SALAAM

MWILI wa aliyekuwa Spika wa Bunge, Samuel Sitta, unarajiwa kuwasili nchini kesho ukitokea  Ujerumani ambako alikuwa akipata matibabu hadi alipofikwa na mauti juzi.

Msemaji wa familia ya marehemu, Gerald Mongella, alisema  mwili huo utawasili Uwanja wa Ndege wa Julius Nyerere (JNIA) saa 8:30 mchana na unategemewa kuwasili nyumbani kwake Mtaa wa Manzese Msasani Dar es Salaam saa 11:30 jioni.

“Ijumaa saa 3:00 asubuhi mwili utaagwa katika Viwanja vya Karimjee na saa 9:00 utasafirishwa kwenda Dodoma ambako wabunge watapata muda wa kutoa heshima zao za mwisho kwa kiongozi huyo kabla ya kusafirishwa kwenda Urambo Tabora kwa mazishi   Jumamosi.

“Kwa wale watakaokuwa wanakwenda Tabora tutakuwa na basi moja kubwa na tukishaaga hapa Dar es Salaam wataondoka moja kwa moja tutakutana huko” alisema Mongella.

Viongozi mbalimbali jana waliendelea kumiminika nyumbani kwa marehemu wakiungana na ndugu kuomboleza kifo cha kiongozi huyo aliyejipatia umaarufu mkubwa wakati akiwa Spika wa Bunge la tisa.

Miongoni mwa waliofika ni mbunge wa zamani wa Kahama, James Lembeli, Mwantumu Mahiza, Dk.Emmanuel Nchimbi, mbunge wa Bunge la Afrika Mashariki, Shyrose Banji, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda na aliyekuwa mbunge wa Zanzibar, Abdulkarim Shaa.

Akimwelezea marehemu, Lembeli alisema Sitta atakumbukwa kwa vuguvugu la kupambana na ufisadi alipokuwa Spika wa Bunge la tisa ambako pia aliweza kuruhusu mijadala migumu bungeni.

“Sidhani kama kuna Spika aliyeweza kulijenga Bunge kama ilivyokuwa kwa Spika Sitta, alikuwa na upendo wa maendeleo kwa kila binadamu,” alisema Lembeli.

Alisema alimfahamu Sitta alipoingia bungeni kwa sababu alimfundisha siasa na kusimamia ukweli na kusimamia alichokiamini.

“Niliingia kwenye siasa kwa bahati mbaya sikuwa naipenda lakini Mzee Sitta alinifundisha ABC za siasa lakini ameondoka ameacha hajakamilisha malengo yake,” alisema.

Naye Emmanual  ole Naiko aliyewahi kufanya kazi na Sitta, alisema atamkubuka   kwa mabadiliko makubwa aliyoyafanya katika Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC).

“Hii ilitubadili na utendaji na ilitubadili fikra hata wawekezaji walipokuwa wanakuja ilikuwa rahisi kupata taarifa na alitusaidia katika maeneo tuliokuwa tunakwama,” alisema ole Naiko.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles