23.7 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

MUHIMBILI NA TEKNOLOJIA YA KUZUIA VIFO VYA GHAFLA

  • Gharama yake ni Sh milioni 30 kwa mgonjwa mmoja

Na VERONICA ROMWALD – DAR ES SALAAM


NI kifaa kidogo mno ukikitazama machoni, ambacho hupachikwa kwa ustadi wa hali ya juu kwa njia ya upasuaji katika moyo wa binadamu ili kumsaidia kuishi.

Licha ya udogo wake wa umbo, kifaa hicho kina uwezo mkubwa wa kusaidia kuzuia kifo cha ghafla kwa mtu anayesumbuliwa na magonjwa ya moyo hasa shinikizo la damu.

Kwa kawaida kifaa hicho hupandikizwa kwa mtu ambaye utendaji kazi wa moyo wake upo chini ya kiwango cha asilimia 50 na wale ambao kiwango chao cha mapigo ya moyo ni chini ya 40 kwa dakika.

Wataalamu wa afya wanasema mara nyingi watu wenye tatizo hilo huanguka ghafla na kwamba hali hiyo husababishwa na kuziba kwa mishipa ya damu.

Wanasema kitendo cha mishipa ya damu kuziba husababisha damu kushindwa kupita kwa wepesi kwenda katika sehemu mbalimbali za mwili.

Hivi majuzi, Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na Taasisi ya Madaktari Afrika ya nchini Marekani ilifanya upasuaji na kuwapandikiza kifaa hicho jumla ya wagonjwa 12.

 

Jinsi unavyofanyika

Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo wa JKCI, Peter Kisenge anasema kabla ya kumfanyia mgonjwa upasuaji wa kupandikiza kifaa hicho, kwanza hufanyia uchunguzi kwa kutumia kipimo maalumu cha ECG.

“Kipimo hicho ndicho ambacho hutupa mwelekeo iwapo mgonjwa husika anapaswa kufanyiwa upasuaji kupandikizwa ICD pacemaker au la,” anabainisha.

Anasisitiza kifaa hicho kina uwezo wa kuzuia kifo cha ghafla hasa kwa wagonjwa ambao wana tatizo la kuziba kwa mishipa ya damu.

“Wagonjwa ambao tunawapandikiza kifaa hiki ni wale ambao utendaji kazi wa mioyo yao ulikuwa upo chini ya kiwango cha asilimia 50, hawa mara nyingi huishiwa nguvu na kujikuta wakianguka ghafla,” anasema.

Anaongeza: “Wagonjwa wengine ambao hupandikizwa kifaa hiki ni wale ambao kiwango cha mapigo yao ya moyo kilikuwa chini ya 40 kwa dakika.

 

Gharama yake ni kubwa

Daktari huyo anasema nchini India upasuaji huo hugharimu hadi Sh milioni 100 kwa kila mgonjwa mmoja kiasi ambacho ni kikubwa.

“Lakini kwa kuwa serikali imefanya uwekezaji mkubwa hapa JKCI, tunafanya upasuaji huo ambapo kila mgonjwa mmoja anagharimu kiasi cha Sh milioni 30, hivyo kwa kuwafanyia upasuaji wagonjwa hao tumeokoa zaidi ya Sh milioni 300 ambazo zingetumika kuwatibu nje ya nchi,” anasema.

Anasema pamoja na wagonjwa hao, wengine wawili wamefanyiwa upasuaji wa kupandikizwa betri maalumu iitwayo kitaalamu CRTD-pacemaker.

Anasema betri hiyo imewekwa kwa wagonjwa ambao baada ya kufanyiwa uchunguzi kwa kutumia kipimo cha ECG waligundulika mapigo yao ya moyo yalikuwa yapo chini mno

“Unaweza kuona ICD – pacemaker na CRTD –pacemaker ni vifaa ambavyo vinafanana lakini kila kimoja kina kazi yake na hadi tunamfanyia upasuaji mgonjwa na kumpandikiza ni lazima tumfanyie uchunguzi kwa kutumia kipimo cha ECG ambacho hutusaidia kujua mgonjwa anastahili kuwekewa kifaa kipi,” anafafanua.

 

Kwanini mishipa huziba

Kwa kawaida binadamu anapofanya shughuli yoyote ile mwili wake huhitaji kiwango fulani cha damu, mahitaji ya kiwango cha damu huongezeka kulingana na shughuli husika anayoifanya kwa wakati huo.

Hata hivyo, iwapo itatokea mwili wa ukahitaji kiwango fulani cha damu lakini kikakosekana moja kwa moja mtu husika hupata matatizo makubwa.

Wataalamu wanaeleza kwamba ili damu ifike katika sehemu mbalimbali za mwili hupita katika mishipa ya damu.

Kwa kawaida mishipa ya damu huwa haipaswi kuwa na mafuta ya aina yoyote, lakini ikiwa kunakuwa na mafuta yoyote yale, husababisha kuziba kwa uwazi unaoruhusu damu kupita.

Wanasema kwa kawaida uwazi huo unapokuwa umezibwa kwa kiwango cha asilimia 50, mtu husika huanza kupata shida mbalimbali.

 

Shida zenyewe

Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo wa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI), Pedro Pallangyo anasema mtu husika hupata maumivu ya kifua.

“Maumivu huwa makali mno hasa katika upande wa kushoto, mtu hata akifanya shughuli ndogo tu hujikuta mwili wake ukichoka haraka,” anabainisha.

Daktari huyo anafafanua kwamba kwa kawaida mtu anapofanya shughuli yoyote mwili wake huhitaji kiwango fulani cha damu na kwamba mahitaji hayo hutofautina kulingana na shughuli anayoifanya kwa wakati huo.

“Sasa unakuta mwili unahitaji damu lakini kwa kuwa mafuta yapo kwenye mishipa ya damu hushindwa kupita kuzunguka kwenye mwili.

“Matokeo yake kadri muda unavyozidi kwenda mbele mafuta yanazidi kutanda kwenye damu hasa kwenye mishipa inayopeleka damu kwenye moyo na kuziba kabisa ule uwazi, matokeo yake mtu hupata shinikizo la damu na wengi hufariki ghafla hasa wanapokuwa usingizini,” anabainisha.

Dk. Pallangyo anasema hali hiyo hutokea pale mishipa ya damu inapokuwa imeziba kwa kiwango cha asilimia 100.

 

Hali ya ugonjwa

Anasema tatizo la kuziba kwa mishipa ya damu enzi za mababu zetu lilionekana kuwaathiri zaidi watu ambao walikuwa na umri wa kuanzia miaka 40 na kuendelea.

Daktari huyo anasema katika miaka ya hivi karibuni, hali ni tofauti kabisa kwani tatizo hilo linaonekana kuwakumba zaidi watu walio na umri wa kuanzia miaka 40 kushuka chini.

Anasema tafiti zinaonesha awali tatizo hilo lilikuwa likiwakumba zaidi watu wanaoishi katika nchi zilizoendelea lakini leo hii linaonekana kuwapo zaidi katika nchi zinazoendelea, Tanzania ikiwamo.

 

Visababishi

Daktari huyo anasema zipo sababu nyingi ambazo husababisha kuziba kwa mishipa ya damu lakini zimegawanyika katika makundi makuu mawili.

“Kuna suala la lishe, tunazungumzia kuhusu ulaji mbovu hasa vyakula vyenye mafuta mengi, uzito kupindukia, kutokufanya mazoezi, unywaji wa pombe kupita kiasi na uvutaji wa sigara,” anasema.

Anasema sababu nyingine huhusisha magonjwa mbalimbali hasa yale ya shinikizo la damu na kisukari.

 

Mgonjwa

Ally Aboud (45) (si jina lake halisi), mwenyeji wa Mkoa wa Tanga ni miongoni mwa wagonjwa wanaosubiri kufanyiwa upasuaji kutibu tatizo la kuziba kwa mishipa ya damu.

Anasema katika maisha yake alikuwa akipendelea mno kuvuta sigara na kwamba hakuwahi kufikiria iwapo zitamfikisha katika hali aliyonayo sasa.

“Nilipenda kuvuta sigara, hata watu waliponishauri niache au hata nipunguze sikuwasikiliza, niliona ni sehemu ya maisha yangu, kwa siku nilikuwa nina uwezo hata wa kumaliza sigara 20,” anasema.

Ally anasema alianza kuvuta sigara alipofikisha umri wa miaka 20 baada ya kushawishiwa na marafiki zake ambao alikuwa akikaa nao kijiweni kila siku jioni.

“Walinishawishi nikaanza kuvuta kidogo kidogo kwa kujificha nyumbani wasijue, lakini kadiri muda ulivyokwenda ndivyo nilivyonogewa na nikaanza  kuitafuta mwenyewe (kununua dukani), kumbe nimejisababishia matatizo,” anasema.

 

Wengi wanaugua

Dk. Pallangyo anasema katika taasisi hiyo kila wiki wanaona wagonjwa zaidi ya 35 wenye tatizo la kuziba kwa mishipa ya damu.

“Iwapo ukikadiria idadi hiyo utaona kwa mwezi tunaona wagonjwa wapatao 140, katika mwaka 2015/16 tuliwafanyia uchunguzi takribani wagonjwa 400 katika mtambo wetu maalumu wa ‘cath lab’,” anasema.

Anasema katika maonesho ya kimataifa ya biashara (sabasaba) waliwafanyia uchunguzi watu 1,375  ambapo asilimia 31 kati yao walikutwa na tatizo la shinikizo la juu la damu.

“Kati ya hao asilimia 39.2 walikutwa na uzito mkubwa, wagonjwa 39 tuliwapa rufaa kuja hapa JKCI, wote walikuja na kati ya hao wagonjwa 31 tuliwakuta na shinikizo la juu la damu na wagonjwa saba wamegundulika wana tatizo la moyo mkubwa, mmoja alikutwa na tatizo kwenye milango ya moyo wake (valve) wameanza kupata matibabu,” anasema.

 

Ushauri

Dk. Pallangyo anashauri ni vema jamii ikaepuka na kuachana na tabia hatarishi zinazosababisha tatizo hilo.

“Visababishi vingi vinaepukika kwa mfano suala la kuacha kuvuta sigara, kufanya mazoezi, kuzingatia ulaji unaofaa ni mambo ambayo yapo ndani ya uwezo wa kila mmoja, ukiacha zile sababu nyinginezo za ugonjwa.

“Tubadilike na kuzingatia mfumo bora wa maisha, kwa sababu gharama ya kutibu tatizo hili ni kubwa, na mara nyingi wale wanaomudu ni wale ambao wana bima ya afya, Wale wasio na bima hushindwa kabisa kumudu.

 

Huduma kusogezwa karibu na jamii

Dk. Kisenge anasema ili kusogeza huduma ya matibabu na afya ya moyo karibu zaidi na jamii, taasisi hiyo sasa imeanza kutoa mafunzo kwa madaktari wa ngazi ya uzamivu.

“Madaktari hao pindi watakapomaliza masomo yao wanatarajiwa kwenda katika Hospitali ya Mloganzila (iliyopo nje kidogo ya jiji la Dar es Salaam na Hospitali ya Benjamini (Dodoma),” anasema.

 

Ushirikiano zaidi

Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo wa Taasisi ya Madaktari Afrika, Mathew Sackett anasema taasisi hiyo ipo tayari kuendelea kushirikiana na JKCI kutoa huduma hiyo.

“Ni mara yangu ya kwanza kuwapo nchini Tanzania, nimefurahi kuona uwekezaji mkubwa uliofanywa na serikali hapa.

“Madaktari Afrika tutaendelea kushirikiana na JKCI kuendelea kutoa mafunzo kwa wataalamu na kufanya upasuaji kuwasaidia wagonjwa ili tuokoe maisha ya wengi zaidi,” anasema.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles