Na Mwandishi Wetu, Mtanzania Digital
Wanachama wa Klabu ya Simba katika eneo la kwa Mkolemba Kata ya Kipunguni wamezindua tawi lao lenye wanachama 300 na kuchangia ujenzi wa choo cha wananchi.
Uzinduzi huo ulifanywa na Meya wa Jiji la Dar es Salaam, Omary Kumbilamoto, ambaye ameahidi kuwanunulia televisheni ili wawe wanaangalia michezo mbalimbali.
“Mmenifurahisha sana hasa mnavyojitoa kusaidia jamii, Jumanne ijayo nawaletea tv muwe mnaangalia ligi,” amesema Kumbilamoto.
Naye Mwenyekiti wa tawi hilo, Daluwesh Swalehe, amesema malengo yao ni kusaidia jamii ambapo kwa kuanzia wametoa mifuko minne ya saruji kuchangia ujenzi wa choo kinachotarajiwa kujengwa katika Mtaa wa Amani.
“Eneo hili kulikuwa hakuna tawi la Simba kwahiyo tumeweka kwa ajili ya kuwarahishia wana Msimbazi wapate huduma, wakitaka kwenda kwenye michezo wanakuwa na uhakika wa usafiri,” amesema Swalehe.
Naye Katibu wa tawi hilo, Yusuph Moshi, amesema anaamini tawi hilo litakuwa mfano na kwamba watafika mbali.
Kuhusu suala la kufukuzwa kocha amesema; “Uongozi uko sahihi kwa sababu tunahitaji mafanikio na kuna vitu vilionekana, tumetoa makocha wangapi na bado tumefanikiwa.