BUNGE, leo litaendelea na vikao vyake mjini hapa huku mjadala wa hotuba ya bajeti ya Waziri Mkuu ukijadiliwa na wabunge.
Wiki iliyopita Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, aliwasilisha bajeti ya Sh bilioni 236.75 kwa ajili ya ofisi yake huku akiapa kuendelea kukomesha udhaifu wote ndani ya Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) kwa mujibu wa sheria.
Alisema hatua hiyo itakwenda sambamba na kuwaondoa watumishi wote wasiokuwa waaminifu ambao wamekuwa wakichangia kupoteza mapato ya Serikali yanayohitajika katika kutoa huduma muhimu kwa wananchi.
Kauli hiyo aliitoa alipokuwa akiwasilisha bajeti ya ofisi yake kwa mwaka wa fedha 2017/17.
Alisema pamoja na hali hiyo, serikali imefanya kazi kubwa ya kuimarisha mifumo ya ukusanyaji mapato ambako malipo yote kwa sasa wanafanyika kupitia benki na kuoanisha mifumo ya Bandari na TRA.
Waziri Mkuu aliwataka wafanyabishara kutambua kwamba Serikali inaendelea kuboresha huduma katika bandari zote hususan ya Dar es Salaam.
“Niwahakikishie wananchi na wafanyabiashara kuwa Serikali itaendelea kuboresha huduma katika bandari zetu na hususan Bandari ya Dar es Salaam kwa kupunguza idadi ya siku za kutoa mizigo bandarini ili tufikie siku mbili au chini ya siku hizo.
“Tutaziondoa kero zote zilizoainishwa na Mawakala wa Forodha nilipokutana nao tarehe 21 Machi, 2016 jijini Dar es Salaam. Vilevile, Serikali itaziba mianya yote ya upotevu wa mapato bandarini na wale wote watakaobainika kushiriki kwenye wizi wa aina yoyote wataondolewa na kuchukuliwa hatua za sheria,” alisema Majaliwa.
Alisema makadirio ya bajeti aliyoiwasilisha ni mwendelezo wa utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi ya mwaka 2015 ambayo imeainisha ahadi ambazo Serikali ya CCM itatekeleza katika miaka mitano ijayo.
“Makadirio ya Bajeti yamezingatia ahadi za Rais Dk. John Magufuli alizotoa wakati wa Kampeni na katika uzinduzi wa Bunge la 11 Nemba 20, mwaka jana.
“Serikali ya Awamu ya Tano imedhamiria kufikia malengo yaliyokusudiwa ya kujenga Taifa imara katika uchumi na maendeleo ya watu katika Kanda ya Afrika Mashariki na Barani Afrika kwa ujumla,” alisema.
Mahakama ya mafisadi
Majaliwa alisema wakati wa uzinduzi wa Bunge Novemba 20 mwaka jana Rais Dk. John Magufuli aliahidi katika mwaka 2016/17, Serikali itaanzisha Mahakama Maalumu ya Ufisadi.