23.3 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

MIMBA ZA UTOTONI BADO JANGA NCHINI

NA OSCAR ASSENGA

KUNA usemi unaosema ukicheka na nyani utavuna mabua, hali hii inajidhihirisha katika matukio ya wanafunzi wa kike kukatishwa masomo

kutokana na kupata ujauzito na kusababisha  kushindwa kufikia ndoto zao za kupata elimu bora ambayo inaweza kuwa mkombozi kwa maisha yao.

Licha ya kuwapo kwa sheria kali za vifungo vya miaka 30 kwa watakaobainika kuhusika kwa namna moja au nyingine kuwapa hali hizo wanafunzi hao,

lakini suala hilo limekuwa wakati mwingine likimalizwa kienyeji na mamlaka husika kutokana na wahusika au jamii fulani inayotajwa kwenye jambo hilo kuamua kukaa na kuyaongea na hatimaye kuweza kuyamaliza.

Jambo hilo limeleta manung’uniko kwa watendewa kwani ni wazi kuwa baada ya kutokea hali hiyo msingi mzima wa maisha yao unakuwa umepotea na kujikuta wakishindwa kujua wafanye nini baada ya kujikuta wakiingia kwenye majukumu ya kuitwa mama bila kutarajia.

Licha ya Serikali ya kuonekana kulipa uzito jambo hilo, lakini yapo baadhi ya maeneo nchini ambayo vitendo hivyo vinatokea na baadaye wahusika kuamua kukaa pamoja na kufikia mwafaka, huku mtendewa akiendelea kubaki hana la kufanya kutokana na ndoto yake kukwamishwa.

Nasema hivyo kwa sababu kama hatua kali zingekuwa zinachukuliwa ipasavyo, hili ambalo limejitokeza kwa Mkoa wa Tanga kuwa na idadi kubwa ya wanafunzi waliopata mimba yaani mimba za utotoni 261, lisingejitokeza kwa kiasi hiki.

Takwimu hizo zilizotolewa hivi karibuni na Ofisa Elimu Taaluma Mkoa wa Tanga, Wiliam Mapunda, zinaonyesha idadi kubwa ya waathirika wa jambo

hilo ni wanafunzi wa shule za sekondari ambapo 206 waliripotiwa kupata ujauzito wakiwa mashuleni.

Huku kwa shule za msingi walioripotiwa walikuwa 55, jambo ambalo ni hatari kwa ukuaji wa taaluma ya elimu mkoani hapa, lakini linaweza kukwamisha nyuma juhudi zinazoweka iwapo halitapatiwa ufumbuzi haraka.

Ni dhahiri kabisa vitendo hivyo iwapo vitafumbiwa macho vinaweza kukatisha ndoto za wanafunzi wengi ambao wanatarajiwa kufanikiwa kupitia elimu hata kuiongoza jamii ya Watanzania.

Wapo baadhi yao walikuwa na ndoto za kuwa siku moja mawaziri, mabalozi na hata viongozi ambao wangeweza kuisaidia jamii kuinuka kiuchumi, hivyo mambo yanapokuwa kinyume chake kutokana na kupata ujauzito ni kuzima malengo yao muhimu.

Lakini sababu kubwa ambayo huenda ikawa inachangia kutokea matukio kama haya ni uwepo wa ngoma za usiku maarufu kama baikoko na vibanda vya video, jambo ambalo limekuwa hatari kwao kutokana na vishawishi.

Jambo kubwa na la msingi ambalo linaweza kusaidia kuondokana na kadhia hiyo ni utungwaji wa sheria kali itakayosaidia jamii hiyo kuweza kusoma bila kuwepo kwa vipingamizi vya aina yoyote ile.

Kwani ni ukweli usiopingika leo hii kwenye maeneo ya vijiji mbalimbali hapa nchini wapo wanafunzi ambao hivi sasa wanajuta kutokana na kukatishwa masomo kutokana na kupata ushawishi kujiingiza kwenye mapenzi na hatimaye kujikuta wakipata ujauzito ambao unakwamisha ndoto zao.

Sambamba na kuchukuliwa hatua kali wahusika, lakini pia lazima kuwepo na sheria ambayo itawabana wanafunzi watakaobanika kuanzisha mahusiano ya kimapenzi, huku wakijua kuwa bado hawajafikia wakati wa kufanya hivyo ili kukomesha tabia hiyo.

Kwani tunaweza kuwakamata vijana ambao wana mahusiano na wanafunzi kumbe ukakuta wao wenyewe ndio washawishi wakubwa kutaka mambo hayo, jambo ambalo linaweza kukwamisha juhudi za kuwaepusha na madhila hayo.

Kama hatua zinachukuliwa kwa wahusika na kuachwa wanafunzi ambao wamekubali kuingia kwenye mahusiano na dhahiri jambo hili hatutaweza kulimaliza.

Lakini pia lazima jamii itambue kuwa jambo kama hilo linapotokea kwenye jamii zao na kuamua kulifumbia macho kwa kuyazungumza kifamilia au kindugu, inachangia mambo ya aina hiyo kuendelea kutokea.

Suala kubwa ambalo limekuwa likiziponza familia nyingi hasa za vijijini kwani wanaona wakimpelekea Polisi muhusika atafungwa miaka 30 na wazazi watamhudumia mtoto, kutokana na hali hiyo wazazi wanaona ni bora vijana hao waoane ili waweze kukaa pamoja na kuwatunza watoto wao, hivyo lazima Serikali ione namna ya kufikisha elimu kwenye maeneo hayo ili vitendo hivyo vimalizike.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles