25.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

MFUKO WA UTT MKOMBOZI KWA WASTAAFU

PATRICIA KIMELEMETA

WASTAAFU wengi wakimaliza muda wao wa utumishi kazini wanajikuta wanaishi kwenye mazingira magumu ya kuomba omba kutokana na kushindwa kuweka fedha kwa ajili ya uzeeni hali inayosababisha kuwarudisha nyuma kimaendeleo.

Tatizo hilo linatokana na mishara midogo wanayopata  na kutokuwa na elimu ya kutosha juu ya uwekezaji katika mfuko wa hifadhi ya  jamii  kwa malipo ya uzeeni  kwa wastaafu.

Mfuko utawasaidia kuweka fedha zao ambazo zitatumika mara baada ya kumaliza muda wa kulitumikia taifa ambao  huanzia umri wa miaka 55 kwa hiari na miaka 60 kwa lazima.

Kutokana na hali hiyo, mfuko wa Jamii ni muhimu kwa kila mwananchi kwa sababu ukiwekeza fedha zako, zinakusaidia katika maisha ya baadaye mara baada ya kufikisha umri wa kustaafu.

Hali hiyo inaweza kukusaidia kutimiza ndoto ulizokusudia katika kipindi chote ulichokuwa kazini, jambo ambalo linaweza kukusaidia kuishi maisha mazuri na yasiyokuwa ya kero na adha kwa ndugu, jamaa zako na marafiki..

Kutokana na hali hiyo, wadau mbalimbali wa mifuko ya hifadhi ya jamii wamekuwa wakiwahimiza wafanyakazi na wananchi kwa ujumla kujiunga na mifuko hiyo ili fedha wanazoziweka ziweze kuwasaidia katika maisha ya baadaye.

Licha ya kuwepo kwa mifuko mingi ya uwekezaji nchini ambayo  yenyewe imeanzisha fao la uzeeni, lakini pia mfuko wa UTT ni miongoni mwa mifuko iliyowekeza kwa aajili ya wastaafu hao.

Mfuko huo unawahimiza wastaafu hao kujitokeza kwa wingi ili kujiunga na fao hilo ambalo litawasaidia katika maisha yao mara baada ya kumaliza ukomo wa utumishi.

Akizungumza na Mwandishi wa makala haya hivi karibuni, Mkurugenzi wa Masoko wa Mfuko wa Uwekezaji wa UTT, Daud Mbaga anasema kuwa, mfuko huo umeanzisha uwekezaji maalumu ambao unaanzia sh 10,000 ili kutoa fursa kwa wastaafu waweze kujitokeza na kuweka fedha zao ambazo zitawasaidia mara baada ya kustaafu kwao.

Anasema, lakini pia kiasi hicho cha fedha kinaweza kutumiwa na mwananchi mwingine yoyote ambaye atatamani kuweka fedha zake kwenye mfuko huo.

“Mfuko wa wastaafu ni muhimu sana kwa kila Mtanzania ili kuweka fedha ambazo zitawasaidia pindi wanapofikisha umri wa kustaafu, hali ambayo inaweza kusaidia kutimiza malengo waliyokusudia yakiwamo ya ujenzi wa nyumba, kusomesha, matibabu na mengineyo,”anasema Mbaga.

Anaongeza, kwa sababu watanzania wapo zaidi ya milioni 45 na wenye uwezo wa kuwekeza kuanzia 10,000 wanaweza kufika milioni 20, hivyo basi wanapaswa kujitokeza na kufanya uwekezaji huo ambao utawasaidia katika maisha ya baadaye.

Anasema kutokana na hali hiyo, vijana waliopo kazini na wale wanaotarajiwa  kupata ajira, wanapaswa kujitokeza UTT na kuweka fedha zao ambazo zitawasaidia katika maisha ya baadaye.

“Ikiwa watanzania milioni 20 wakijtokeza na kuwekeza kwa kila mmoja kuweka sh 10,000, tutakuwa tumewekeza sh bilioni 200, hali ambayo inaweza kumsaidia mstaafu kupata fedha nyingi pindi anapoamua kuchukua fedha zake,”anasema mbaga.

Anaongeza, kwa sababu vipato vya wananchi vinatofautiana, hivyo basi kila mmoja anapaswa kuwekeza kulingana na uwezo wake.

Anasema wapo wanaoweza kuwekeza kuanzia sh 10,000 au zaidi kulingana na kipato cha mtu, lakini pia uwekezaji huo unaweza kuwanufaisha katika maisha yao na serikali kwa ujumla.

Anasema hivyo basi ni wakati muafaka wa kila mwananchi kuona umuhimu wa kuwekeza kwenye mfuko huo ambao utakuwa mkombozi katika maisha ya baadaye kutokana na kupanda kwa gharama za uendeshaji wa maisha ya kila siku hasa katika kipindi hiki cha sayansi na teknolojia.

Anasema  licha ya kuwepo kwa mfuko huo, lakini pia kuna uwekezaji wa pamoja ambao unaweza kushirikisha makampuni mbalimbali kukusanya fedha chini ya makubaliano maalumu na kumpa fedha hizo meneja ili aweze kuzisimamia kwa kufuata makubaliano ya awali yatakayotokana na wadau husika.

Anasema, fedha hizo zitawekwa kiutaalamu kwenye masoko ya fedha na masoko ya mitaji kama vile hisa na kusimamiwa na mamlaka husika ikiwamo Mamlaka ya Masoko ya Hisa na Mitaji (CMSA) ili kuhakikisha kuwa uwekezaji huo unakua salama na wala hakuna mtu atakayedhurumiwa haki yake.

Anasema lakini fedha hizo zitasimamiwa na taasisi za kifedha zikiwamo mabenki na dhamana mbalimbali kwa sababu wao ndiyo muhimu katika uwekezaji wa fedha.

“Fedha hizo zitakaguliwa na wakaguzi wa hesabu akiwemo Mkaguzi Mkuu  wa Serikali ambaye ndiyo mwenye jukumu la kuangalia mahesabu kama yako sahihi wakiwa pamoja na wanasheria ambao husimamia mikataba ya uwekezaji ili kuhakikisha kama taratibu za kisheria zilifuatwa,”anasema.

Anaongeza hivyo basi wawekezaji hukaa kila mwaka  pamoja na meneja (UTT AMIS) ili kutathimini maendeleo ya Uwekezaji na kufanya maboresho ambayo yataleta tija.

Anasema kutokana na hali hiyo mstaafu pia anaweza kujiunga kupitia utaratibu huo ambao utamsaidia kupata fedha kwa ajili ya maisha ya baadaye.

Anasema hali hiyo inaweza kuwasaidia furaha na amani huku ukijua kuwa, fedha za kutumia katika maisha yao ya baadaye zipo na wala huwezi kuishi kwenye maisha magumu.

Anasema kwa sababu kila mstaafu anakadiriwa kuwa na umri wa kuanzia miaka 60 au zaidi, hivyo basi hata uwezo wa kufanya kazi unapungua kutokana na kuchoka kwa viungo vya mwili, jambo ambalo linaweza kumfanya kushindwa kutimiza majukumu yake ipasavyo.

Anasema kutokana na hali hiyo  fedha atakazopewa katika mfuko huo zinakusaidia kupata faida ambayo itakusaidia maishani.

Anasema kutokana na hali hiyo, wastaafu hao wanaweza kuchagua mfuko wanaoona unafaa katika uwekezaji huo ili waweze kupata faida kubwa itakayowasaia kuendesha maisha.

“UTT tuna mifuko mingi ya uwekezaji ambayo mstaafu anaweza kuchagua na kujiunga nayo kwa ajili ya kuweka fedha zake ili ziweze kumsaidia katika maisha ya baadaye,”anasema.

Anasema hali hiyo inaweza kuwaondoa kwenye kundi la kulelewa au kuombaomba kutokana na kujiwekea akiba ya uzeeni, jambo ambalo linaweza kupunguza utegemezi kwa watoto au familia.

Anasema mkakati uliopo ni kuhakikisha kuwa, wanatoa elimu kwa watumishi wa serikali, sekta binafsi na wadau mbalimbali ili waweze kujiunga na mfuko wastaafu ambao utawasaidia katika maisha ya baadaye.

Anasema lakini pia mfuko huo utakua mkombozi kwa wawekezaji kutokana na kupata faida ambayo inaweza kuwakwamua kiuchumi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles