25.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Mbowe atoboa siri uteuzi Dk. Mashinji

mashinjiNa Fredrick Katulanda, Mwanza

MWENYEKITI wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe ametoboa siri ya kumteua Dk. Vincet Mashinji kuwa Katibu Mkuu wa chama hicho.

Mbowe alisema amemteua Dk. Mashinji kutokana na kiwango chaka cha elimu pamoja na ushujaa wake wa kupambania maslahi ya madaktari kwa kuitisha migomo.

Akihutubia maelefu ya wakazi wa Jiji la Mwanza jana katika viwanja vya Furahisha wakati wa kumtambulisha kiongozi huyo, Mbowe alisema Chadema imemteua Dk. Mashinji kutokana na sifa, uwezo na si kwa sababu ya ukabila.

Alisema kwa uteuzi huo, ametoa somo kwa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwa kuteua mtu ambaye baba yake si kigogo wa chama, tofauti na wao ambao wamekuwa wakitoa nafasi kwa watoto wa vigogo au kwa misingi ya rushwa.

Alisema Dk. Mashinji ana kiwango cha juu cha elimu na si mwoga jambo ambalo anaamini litamsaidia kuendesha chama.

“Baada ya kupekuwa historia yake tulibaini ni mmoja wa wale walioanzisha mgomo wa madaktari nchi nzima, kisha akafukuzwa akiwa na wenzake kina Dk. Steven Ulimboka.

“Tulipogundua aliongoza mgomo tulijua si mwoga, kama alikomaa kutetea maslahi ya madaktari na wenzake, basi tuliona anafaa kukomaa kutetea Watanzania… si mtoto wa Mbowe wala mtoto wa Lowassa (Edward).

“Tumeamua kumteua mtu mwenye sifa na uwezo pamoja na karama za uongozi, tumemwibua kutoka chini, angekuwa CCM angelazimika kuhonga mpaka ndugu zake ili ashinde  nafasi hii,” alisema.

Alisema uteuzi huo, unaonyesha dhamira ya Chadema ya kugawana madaraka na kubainisha ndani ya Kamati Kuu wapo watu ambao wana sifa za kuwa makatibu wakuu, lakini wana majukumu mengine.

Alisema wamekubaliana walioko bungeni waendele kupambana huko ili mambo mengine yafanywe na katibu.

 

Dk. Mashinji

Kwa upande wake, Dk. Mashinji akizungumza baada ya kutambulishwa, alisema jukumu la kwanza ambalo linamkabili ni kujenga chama hicho kimkakati.

Alisema atafanya kazi zake kisasa kwa lengo la kuongeza ufanisi.

Alisema tayari ametoa maelekezo kwa madiwani wa Chadema katika halmshauri zote kuanza kuunda kamati za ufuatiliaji za wananchi ambazo zitakua na jukumu la kufuatilia utendaji na utekelezaji na maendeleo kwa kata husika.

“Huu ndiyo mkakati wangu wa kwanza naanza kuutoa hapa, umebeba lengo la la kuisukuma Chadema mbele na kufanikisha kushinda na kushika dola mwaka 2020.

 

Lowassa

Kwa upande wake, aliyekuwa mgombea wa urais kwa tiketi ya chama hicho, Edward Lowassa aliwashukuru wananchi wa Mwanza kwa kumpigia kura wakati wa Uchaguzi Mkuu mwaka jana.

Alisema kura nyingi alizopata ni kielelezo cha kukubalika kwa wananchi hao, japokuwa waliotangaza walisema hazikutosha.

Alisema imani yake ni kujipanga zaidi ili mwaka 2020 washike dola na kwamba wamepata katibu mkuu mpya kijana ambaye atasimamia chama vilivyo na  anaamini watafanya vizuri zaidi.

 

Wenje

Akizungumzia uchaguzi, aliyekuwa Mbunge wa Jimbo la Nyamagana, Ezekiel Wenje alisema kulingana na matokeo yalivyo, japo Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), haikumtangaza anatambua yeye ndiye mshindi na ndiyo maana amekwenda mahakamani kufungua kesi.

Aliomba wafuasi wa chama hicho kumwombea, wakati huu ambao kesi yake inaendelea kusikilizwa mahakamani.

“Ukitaka kujua nani kashinda tupite mtaani mimi na huyo Mbunge wa CCM (Stanslaus Mabula), utaona yeye anatembea na polisi, mimi napita nakatiza mitaa, hii maana yake aliyetangazwa anatembea na hofu ya Mungu,” alisema.

 

Mwalimu

Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu (Zanzibar ) Salum Mwalimu alisema uteuzi wa Dk. Mashinji umeonyesha ukomavu ndani ya chama na namna ambavyo inaweza kuibua watu wenye karama za uongozi.

“Niseme CCM imezoea kununua watu wa upinzani, kila ikinunua sisi tutaibua wapya kama tulivyofanya kwa Dk. Mashinji,” alisema.

 

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles