ASIFIWE GEORGE NA RUTH MNKENI, DAR ES SALAAM
UONGOZI wa Soko la Kariakoo jijini Dar es Salaam, umepiga marufuku magari yanayoingiza mazao ya chakula yaliyofungashwa kwa kutumia majani.
Akizungumza jijini Dar es Salaam jana, Meneja wa soko hilo, Florens Seiya, alisema wametoa maagizo hayo kwa wafanyabiashara wote wanaoingiza mazao katika soko hilo.
Alisema gari litakalopeleka mazao yaliyofungashwa kwa kutumia majani halitaruhusiwa kuingia ndani ya soko hilo na mazao hayo hayatapokewa.
“Kuanzia Januari 31 ndiyo mwisho wa kupokea magari yaliyobeba mazao yaliyofungshwa kwa kutumia majani ambayo kwa kiasi kikubwa huchangia uchafuzi wa mazingira na kusababisha kuzalisha taka nyingi, hivyo kushindwa kuziondosha kwa wakati.
“Awali nyanya zilikuwa zikisafirishwa zikiwa zimefungashwa kwa majani, lakini sasa imetumika teknolojia nzuri ya maboksi hali inayosababisha nyanya hizo kusafirishwa vizuri bila uharibifu wowote na kupunguza uchafu ndani ya soko, hivyo ni vyema ikatumika teknolojia hiyo katika mazao mengine kama vike, ndizi, parachichi na mengineyo,” alisema Seiya.
Alisema kuanzia Februari mosi gari lolote kutoka mikoani litakaloingiza mazao yalivyofungashwa kwa kutumia majani halitaruhusiwa kuingia katika soko hilo wala bidhaa zake hazitapokewa.
Seiya alisema kwa sasa wameboresha usafi wa mazingira katika soko hilo na wametoa maagizo kwa wafanyabiashara wote kuwa na kifaa maalumu cha kukusanyia taka wanazozalisha wakati wanapoendelea na biashara zao.
Alisema wanaendelea kutoa elimu kwa wafanyabiashara namna ya kutunza mazingiza ikiwa ni utekelezaji wa agizo la Serikali.