30.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Mayanja, Bakari Shime watambiana

mayanja+pichaNA THERESIA GASPER, DAR ES SALAAM

MAKOCHA wa timu za Simba na Mgambo Shooting, Jackson Mayanja na Bakari Shime, kila mmoja ametamba kutoka na ushindi katika mchezo wao wa Ligi Kuu Tanzania Bara mzunguko wa pili utakaochezwa kesho Uwanja wa Taifa Dar es Salaam.

Simba inakutana na Mgambo ikiwa na kumbukumbu ya kuifunga mabao 2-0, katika mchezo wao wa mzunguzo wa kwanza Uwanja wa Mkwakwani, lakini pia mchezo uliopita Simba ilifanikiwa kutoa kichapo cha mabao 4-0 dhidi ya African Sports mchezo uliochezwa Uwanja wa Taifa Dar es Salaam, wakati Mgambo walitoa sare ya bao 1-1, dhidi ya Ndanda FC Tanga.

Akizungumza na MTANZANIA, Mayanja ambaye ni mwenyeji wa mchezo huo alisema hawezi kuidharau timu hiyo ila atakuwa makini kuhakikisha wanawakabili wapinzani wao Mgambo Shooting.

“Katika mchezo lolote linaweza kutokea, hivyo hatuwezi kubweteka badala yake tutaendelea kujipanga ili kupata matokeo mazuri kwenye mchezo huo.

“Hatuwezi kuidharau timu yoyote hata kama ndogo kwa sababu zote zinashiriki Ligi Kuu, hakuna anayetaka kupata matokeo mabaya tutaendelea kufanya vizuri ili kuzidi kupanda juu zaidi,” alisema.

Alisema wanaendelea na mazoezi ili kuyafanyia kazi mapungufu aliyoyaona kwenye mchezo uliopita yasijirudie tena kwenye mchezo huo unaowakabili mbele yao, huku wachezaji wake wakizidi kumpa matumaini kutokana na kufuata yale ambayo anawaelekeza kufanya na kuzidi kufanikiwa kupata matokeo mazuri.

Kwa upande wake, Shime amesema licha ya timu yake kucheza ugenini,  hawatakuwa tayari kuona wanapoteza mchezo huo.

Alisema watahakikisha wanapambana kwenye mchezo huo ili waondoke na pointi tatu muhimu.

“Matokeo mazuri yanapatikana popote pale, sio kama unapocheza ugenini  mchezo ndio unakuwa mgumu si kweli, sisi tumejiandaa kwenye mazingira ya kuchezea popote pale na sasa tupo njiani kuelekea Dar es Salaam kwa ajili ya maandalizi ya mwisho ya mchezo huo,” alisema.

Alieleza Simba ni timu kubwa, lakini haiwezi kuwazuia wao kufanya vizuri kutokana na alivyokiandaa kikosi chake ambapo ameyafanyia kazi mapungufu yaliyokuwa kwenye kikosi.

Mpaka sasa Mgambo Shooting inashikilia nafasi ya nane huku ikiwa imejikusanyia pointi 17 sawa na Toto Africans zikiwa zimetofautiana kwa mabao ya kufunga na kufungana.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles