30.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Mapambano dhidi ya Ukimwi; Serikali kuja na mkakati wa kudhibiti mila hatarishi

Na Mwandishi Wetu, Mtanzania Digital

Serikali imetaka kufanyika kwa utafiti kuhusu mila mbalimbali zilizopo nchini lengo likiwa ni kuondoa zilizo hatarishi kwa jamii ambazo zimekuwa ni chanzo cha maambukizi ya Virusi Vya Ukimwi.

Hayo yamebainishwa jana jijini Dodoma na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Jenista Mhagama, wakati wakujadili changamoto za ukatili wa kijinsia, usawa wa kijinsia, mila potofu na unyanyasaji wa kijinsia katika mwitikio wa mapambano ya VVU na Ukimwi nchini.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Jenista Mhagama, akizungumza wakati wa kikao hicho.

Waziri Mhagama amesema kwa kufanya hivyo kutasaidia kuendelezwa na kutangazwa kwa mila nzuri ikiwa ni pamoja na kutoa elimu katika jamii.

“Kutokana na changamoto ambazo zimekuwa zikijitokeza sababu ya mila, niwakati sasa wakufanya tafiti ili kujua ni zipi ambazo ni nzuri ili zieweze kuendelezwa na elimu ya kutosha kwa jamii itolewe na zile ambazo ni hatarishi ziachwe.

“Lakini pamoja na hayo tuangalie ni kwa namna gani utafiti huo utakuja na mwenendo mzima wa mila nchini kwasasa. Aidha, kuwepo kwa mkakati wa kushirikisha wanaume katika kupima VVU,” amesema Mhagama.

Waziri Mhagama alitoa wito huo baada ya Wasilisho la Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa TACAIDS, Dk. Jerome Kamwela, ambaye amesema kuwa kumekuwa na kiwango kikubwa cha maambukizi ya VVU miongoni mwa wanawake ikilinganishwa na wanaume.

Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa TACAIDS, Dk. Jerome Kamwela.

Aidha, Dk. Kamwela amesema kuwa baadhi ya sababu zinazoelezwa kuchangia kuwaweka wanawake na wasichana balehe katika hatari kubwa ya maambukizi ni pamoja na kushamiri kwa mila hatarishi na mifumo ya kijamii na kiuchumi inayowabagua wanawake na wasichana

“Miongoni mwa changamoto ni pamoja na baadhi ya jamii kuendelea kutekeleza vitendo vya ukatili wa kijinsia kama ukeketaji, ndoa zisizo za hiari na za utotoni.

“Pia kuna kukosekana kwa usawa wa kijinsia katika mgawanyo wa fursa za kiuchumi kunakopelekea wanawake wengi kuwa maskini wa kipato, lakini pamoja na mambo mengine kunatakiwa kuwapo na mkakati wa kushirikisha wanaume,”amesema Dk. Kamwela.

Amezitaja baadhi ya mila hizo kuwa ni pamoja na Ndoa za Mitala / Ndoa za Wake wengi, Ndoa bila ya Utaratibu/Chomolea/ Nyumba nthobu na Makwava, Sherehe za Kijamii, ngoma za Unyago/Usiku, Sherehe za Rika (Mkesha), Disko Vumbi, Chagulaga, Kutakasa wajane na Mila ya kufanya watoto wakishakuwa kulala nje ya makazi ya wazazi.

Akitolea mfano ukeketaji Dk. Kamwela amaesema kuwa baadhi ya maeneo ambayo yameonekana kuendeleza sana kasi ya mila ya ukeketaji hapa Tanzania ni pamoja na mikoa ya kanda ya kati (Dodoma na Singida), Mikoa ya kaskazini: Arusha na Manyara na Kanda ya Ziwa hususan mkoa wa Mara.

“Lakini katika mikoa ya Dodoma na Njombe kuna wazazi wa kiume kufanya Ngono na binti zao au Mzazi wa Kike kufanya mapenzi na mtoto wake wa kiume (MAKWAVA). Asilimia 95 ya wanawake wanaamini kwamba ukeketaji haukubaliki katika imani za dini zao na wametaka utekelezwaji wa mila hii ukomeshwe,”amesema Dk. Kamwela.

Dk. Kamwela ameyataja baadhi ya mafanikio yaliyofikiwa hadi sasa kuwa ni Kufanya uchambuzi wa masuala ya jinsia kuhusiana na UKIMWI ili kujua hali halisi na  kuandaa mipango mipya ya kukabiliana na changamoto za  kukosekana  usawa wa kijinsia.

“Miradi ya DREAMS na AGYW imeendelea kuwajengea uwezo wasichana balehe na wanawake vijana kwenye nyanja za kiuchumi, kielimu na kimabadiliko ya tabia. Afua za haki za binaadamu zimekuwa zikifanyika kuwajengea uwezo watu wanaoishi na VVU, Watunga sheria, Polisi na makundi mbalimbali ya jamii,” amesema Dk. Kamwela.

Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI, Kifua Kikuu, Dawa za Kulevya na Magonjwa yasioambukiza, Fatma Hassan Toufiq.

Upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI, Kifua Kikuu, Dawa za Kulevya na Magonjwa yasioambukiza, Fatma Hassan Toufiq, amesema kuwa kunatakiwa kuwapo na mkakati wa vyombo vya Habari katika kuhakikisha kuwa vinaripoti juu ya Jinsia na Ukimwi ili kuwafikia watu waliowengi zaidi hasa vijana.

“Lakini pia niwakati sasa kwa wanawake kutumika katika kuhamasisha wenza wao kufanya tohara,”amesema Toufiq.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles